Habari

EACC yapokea kesi 44 za ufisadi 

Na NDUBI MOTURI June 4th, 2025 Kusoma ni dakika: 1

TUME ya Maadili na Kupambana na Ufisadi nchini (EACC) imechunguza na kukamilisha kesi 44 kuhusu makosa yanayohusiana na ufisadi na kuyapeleka kwa ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma  (ODPP).

Kati ya kesi hizo 44, ni nne pekee ambazo zimeidhinishwa kufunguliwa mashtaka.

Uchambuzi wa ripoti ya robo mwaka ya tume hiyo unaonyesha kwamba kesi nyingi zinazohusisha kiasi kikubwa cha fedha za umma zilipendekezwa kufungwa (2), zilirejeshwa kwa uchunguzi zaidi (8) na 28 bado zinasubiri meelekeo.
Miongoni mwa zilizoidhinishwa ni kesi mbili zinazohusu kughushi vyeti vya KCSE na wafanyikazi wa Kampuni ya Majisafi na Majitaka ya Nairobi.
Mmoja anafanya kazi kama msaidizi wa usalama, na mwingine kama msaidizi wa kukusanya mapato.
Pia iliyoidhinishwa ni kesi dhidi ya afisa wa polisi katika Kituo cha Polisi cha Capitol Hill ambaye anashtakiwa kwa kupokea hongo ya Sh5,000 ili kuachilia pikipiki iliyozuiliwa.
Kesi nyingine inamhusu msaidizi wa karani wa mahakama katika Mahakama ya Sheria ya Makadara ambaye anadaiwa kupokea Sh50,000 kutoka kwa mlalamikaji ili kuwezesha uchapaji wa kesi inayohusiana na kesi ya jinai.
Hata hivyo, juhudi za kufikia ofisi ya DPP kuhusu maoni yake ya idadi ndogo ya faili zilizoidhinishwa kufunguliwa mashtaka haikufua dafu.
Miongoni mwa wale ambao bado wanasubiri jibu ni mapendekezo ya hali ya juu ya kumshtaki aliyekuwa Katibu Mkuu wa Michezo Kirimi Kaberia na watu wengine watatu kuhusu ubadhirifu wa Sh1.5 bilioni.