Wito wa amani, umoja watawala Sikukuu ya Idd
MAELFU ya waumini wa Kiislamu walikusanyika katika misikiti na viwanja mbalimbali nchini kusherehekea sikukuu ya Eid-ul-Adha huku viongozi wa dini na serikali wakitoa wito wa amani, mshikamano na kuwajali wasiojiweza.
Katika jumbe zao, viongozi waliwataka Waislamu kutumia kipindi hiki kitakatifu si tu kwa sherehe bali pia kutafakari, kusaidiana na kudumisha maadili ya Kiislamu.
“Tunawasihi Waislamu kuwakumbuka wahitaji katika kipindi hiki. Idd ni wakati wa kutoa, kuunganisha jamii na kutenda mema,” alisema Sheikh Juma Ngao, Mwenyekiti wa Baraza la Ushauri kwa Waislamu nchini (KEMNAC).
Sheikh Ngao pia aliwahimiza Waislamu kuheshimu afisi ya Kadhi Mkuu akisema taasisi hiyo ni nguzo muhimu ya uongozi wa Kiislamu nchini.
Katika Msikiti wa Jamia katikati mwa jiji la Mombasa, Imam Sheikh Jamaludin Osman alituma ujumbe wa amani na heri kwa Waislamu wote na taifa kwa jumla.
“Huu ni wakati wa unyenyekevu, kutafakari na kueneza mema. Tuwe wajumbe wa amani na matumaini kwa wote,” alisema baada ya kuongoza maelfu ya waumini katika swala ya Idd.
Huku Waislamu wakiendelea na sherehe, viongozi wa Kiislamu walipata nafasi ya kumkosoa Mbunge wa Kilifi kaskazini Owen Baya, kwa kuondoa mswada wake bungeni uliolenga kutangaza Muguka kuwa dawa hatari.
Sheikh Abu Katada alieleza masikitiko yake akisema viongozi wanapaswa kuangazia mambo yanayowanufaisha wananchi na si maslahi yao binafsi.
Viongozi hao pia walikemea lugha za matusi miongoni mwa wanasiasa wakisisitiza haja ya kuheshimiana licha ya tofauti za kisiasa.
Kamishna wa Kaunti ya Mombasa Bw Mohammed Noor alisema serikali imeimarisha usalama katika maeneo yote ya burudani na bustani ili kuhakikisha usalama wakati wa sherehe.
Sherehe za Idd-ul-Adha zinatarajiwa kuendelea hadi mwisho wa wiki huku familia nyingi zikiendeleza shughuli ya kuchinja wanyama na kugawana nyama na wale wasiobahatika.
Imamu wa Msikiti wa Eldoret Jamia Hussein Mohammed aliwaonya wanasiasa dhidi ya kampeni za mapema huku akitoa changamoto kwa Tume ya Kitaifa ya Uwiano na Utangamano NCIC kuweka mikakati muafaka kukabiliana na wanasiasa wachochezi bila mapendeleo.
“Kampeni za mapema na siasa ambazo tumeanza kushuhudia katika nchi yetu ni tishio kwa umoja wa kitaifa. Ni mapema mno kwa viongozi wetu kuanza kampeni za Uchaguzi Mkuu wa 2027. Huu ni wakati wa kutoa huduma kwa Wakenya wote bila kujali itikadi zao za kisiasa,” alisema Imam Mohammed.
Bw Mohammed alimtaka Rais William Ruto kuzingatia ahadi zake za kampeini za uchaguzi mkuu wa 2022 badala ya kulumbana na upinzani katika siasa za maneno. ‘Tuna nchi nzuri ambayo tunapaswa kuilinda kwa kila njia ili kudumisha amani na utulivu. Lazima tushirikiane kama nchi na kuepuka siasa za ukabila na ubaguzi ili kuchochea maendeleo ya nchi yetu,’ alisema Bw Mohamed.