Kilimo cha nafaka ndogo
KADRI athari za mabadiliko ya tabianchi zinavyozidi kutishia uzalishaji wa mazao ya kawaida kama vile mahindi, ngano na mchele, baadhi ya wakulima na wataalamu wanatafuta suluhu kuhakikisha usalama wa chakula nchini unaangaziwa.
Miongoni mwao ni Dkt Ndungu Kabare, mhadhiri wa zamani Chuo Kikuu cha Karatina, ambaye amejitosa katika uhamasishaji wa kilimo cha nafaka ndogo na mazao yanayostahimili ukame.
Katika shamba lake la ekari tatu lililoko Ruiru, Kaunti ya Kiambu, Dkt Kabare analima mazao kama mtama, wimbi, teff, chia, flax, amaranth maarufu kama mchicha au terere, ndengu na butter beans – maharagwe asilia yanayojulikana kama noe.
“Kwa sasa, ninafanya majaribio ya quinoa na buckwheat, mazao yanayojulikana kwa uwezo wake kustahimili athari za mabadiliko ya tabianchi haswa ukame,” anaelezea mkulima huyu.

Kulingana naye, nafaka na mbegu ndogo kiumbo yana virutubisho vingi, huhitaji maji kiasi tu na hukomaa kwa muda mfupi ikilinganishwa na mazao makuu yanayotegemewa na wengi. “Sifa hizi zinayafanya kuwa muhimu katika kukabiliana na changamoto za ukame na upungufu wa chakula unaosababishwa na mabadiliko ya tabianchi,” anasema.
Baada ya kuacha taaluma ya ualimu wa biashara ya kilimo, Dkt Kabare alianzisha Imani Park Gardens, ambayo baadaye iligeuka kuwa kituo cha mafunzo na majaribio ya kilimo endelevu na himilivu kwa tabianchi.
“Nimekuwa nikishirikiana na Shirika la Utafiti wa Masuala ya Kilimo na Maendeleo ya Mifugo (KALRO), Katumani, Machakos tangu mwaka 2023,” anadokeza. Aidha, taasisi hiyo imekuwa ikimsambazia mbegu bora.
Takwimu kutoka majaribio ya shambani kufuatia utafiti aliofanya Kabare kwa ushirikiano na KALRO zinaonyesha kuwa mtama unaweza kuzalisha kati ya kilo 1,200 na 1,900 katika ekari, huku chia ikizalisha karibu kilo 600.

Hii inaweza kumsaidia mkulima kupata mapato ya hadi Sh180,000 kwa ekari ya mtama na hata Sh600,000 kwa ekari ya chia.
Hata ingawa changamoto kama ndege waharibifu na uhaba wa mashine za kuvuna bado zipo, Dkt Kabare anaamini mbegu na nafaka ndogo zinaweza kuwa nguzo muhimu ya usalama wa chakula na lishe nchini, hasa katika maeneo kame na nusu-kame (ASAL).
Kupitia mafunzo yake, anahamasisha wakulima kukumbatia mazao haya kama njia ya kuboresha kilimo.