Rekodi ya kutisha ya ukatili wa polisi katika serikali ya Ruto kamwe haikomi
KIFO cha mwalimu na mwanablogu Albert Ojwag Jumapili baada ya kukamatwa na maafisa wa usalama kinaongeza lawama kwa utawala wa Rais William Ruto kwa ukiukaji wa haki za binadamu na ukosefu wa uvumilivu wa kisiasa, hali inayotilia shaka ahadi yake ya kuheshimu utawala wa sheria na demokrasia.
Badala ya kutimiza ahadi zake za kulinda uhuru wa raia na kumaliza ukatili wa polisi, serikali yake imelaumiwa kwa kutumia hofu, vitisho na matumizi mabaya ya idara za usalama ili kuzima wanaomkosoa.
Ojwag alikamatwa kwa dai la kutusi mtu mkubwa kupitia anwani zake za mitandao ya kijamii.
Alikamatwa akiwa Migori na kusafirishwa hadi Nairobi anakodaiwa kufariki mikononi mwa maafisa wa polisi.
Mashirika ya haki za binadamu yameripoti ongezeko kubwa la ukiukaji wa haki. Kulingana na Tume ya Kitaifa ya Haki za Binadamu (KNCHR), watu 82 walitekwa nyara kati ya Juni 2024 na kufikia sasa 29 bado hawajulikani walipo.
Ripoti ya Missing Voices ilibaini kuwa watu 104 waliuawa kiholela na polisi mwaka wa 2024 pekee.
Kaunti zilizoathiriwa zaidi ni pamoja na Nairobi (vifo 38), Kiambu, na Migori, huku miezi ya Juni hadi Agosti 2024 ikirekodi mauaji mengi zaidi.
Aidha, miili 50 yenye majeraha ya risasi haijadaiwa katika mochari mbalimbali za umma.
Kisa kama cha Rose Njeri, mwanaharakati wa mtandaoni aliyeunda jukwaa la kupinga Mswada wa Fedha 2025, kimesababisha hofu kubwa.
Alikamatwa na maafisa wanaoshukiwa kutoka Idara ya Upelelezi (DCI), hali iliyoibua shutuma za kunyamazisha uhuru wa kiraia.
Aliyekuwa naibu rais Rigathi Gachagua, ambaye sasa ni mkosoaji mkubwa wa serikali, alitaja hatua hiyo kuwa “jaribio la kukandamiza sauti za vijana” na akaonya kuwa serikali “haijajifunza chochote” kutoka kwa maandamano ya Gen Z mwaka wa 2024 yaliyosababisha vifo vya angalau vijana 60.
Rais Ruto alikuwa ameahidi kuvunja vikosi haramu vya polisi, kusitisha mauaji ya kiholela, na kuanzisha mahakama maalum ya kushughulikia visa vya kutoweka kwa watu.
Ingawa alivunja rasmi Kikosi cha Huduma Maalum (SSU), ukatili umeendelea.Badala ya kupungua, kukamatwa kwa watu kiholela na mauaji yameongezeka.
Waliotekwa ni pamoja na wanaharakati dijitali kama Billy Mwangi, Peter Muteti, Bernard Kavuli na Rooney Kiplangat.
Rais Ruto amekanusha mara kwa mara kuwa anahusika na visa hivyo, akisema mwaka 2024 kuwa: “Sina hata jina moja la mtu aliyetekwa au kupotea.”
Hata hivyo, baadaye alikiri kuwepo kwa visa hivyo na kuahidi kuvimaliza.Wakati wa maombi ya kitaifa wiki mbili zilizopita, Ruto aliomba msamaha kwa vijana: “Kwa watoto wetu, kama kumekuwepo na makosa yoyote, tunaomba msamaha.”
Lakini msamaha huo haukuonekana kuwa wa dhati. Rais Ruto, amekuwa akishambulia mahakama akiilaumu kwa kuzuia miradi ya serikali kupitia maamuzi ya kuizima.
Alitoa kauli za kutishia kutotii maagizo ya mahakama, kinyume na msimamo wake wa 2020 aliposema “kutoheshimu maagizo ya mahakama ni kuingiza nchi kwenye giza na ghasia.”