Habari za Kitaifa

Mbadi: Nimeunda bajeti kwa uangalifu mkubwa, sijaleta ushuru mpya

Na BENSON MATHEKA June 13th, 2025 Kusoma ni dakika: 3

BAJETI ya mwaka wa kifedha 2025/2026 iliyosomwa Bungeni na Waziri wa Fedha John Mbadi jana, ilionekana kulenga kupapasa Wakenya ambao walikasirishwa na ile ya mwaka jana iliyowaongezea mzigo wa ushuru.

Kwa uangalifu, Bw Mbadi hakutangaza hatua za kuongeza ushuru au kupendekeza ushuru mpya wakati ambao serikali itatakiwa kukopa zaidi ya Sh690 bilioni kujaza pengo katika mapato na kulipa madeni.

Tofauti na bajeti za awali, Bw Mbadi hakutangaza hatua za ushuru kwa bidhaa au huduma zozote huku akisema serikali imeweka mikakati ya kuimarisha ukusanyaji wa ushuru.

“Sitapendekeza nyongeza ya ushuru au kuanzisha ushuru mpya katika bajeti ya mwaka huu,” Bw Mbadi alisema na huku akikiri kwamba “Wakenya wameelezea wasiwasi kuhusu deni la umma. Kwa hakika, kuna mtazamo wa ukosefu wa uwazi katika usimamizi wa deni hilo. Kwa hivyo, ninaomba Mkaguzi Mkuu afanye ukaguzi kamili wa deni la taifa.”

Mbele ya Bunge huku wananchi wakifuatilia bajeti yake ya kwanza, Bw Mbadi alionekana kufuata mkondo tofauti na mtangulizi wake katika utawala wa Kenya Kwanza Profesa Njuguna Ndungu ambaye alitangaza ushuru uliozua maandamano makubwa kuwahi kutokea Kenya ya kupinga Mswada wa Fedha.

“Hakuna maisha yanayopaswa kupotea, wala mali kuharibiwa tena. Ujumbe kutoka kwa Wakenya uko wazi. Tangu nichukue wadhifa huu, nimeahidi kupunguza mzigo wa ushuru. Kwa hivyo, Mswada wa Fedha 2025 haupendekezi ushuru mpya wala kuongeza viwango vya sasa,” alisema Bw Mbadi.

Ingawa alisawiri bajeti hii kuwa ya matumaini ,haina mabadiliko makubwa kwa Wakenya wa kawaida kwa kuwa haigusi mizizi ya matatizo yao kama vile ushuru wa nyumba na ada nyingine dhalimu.

Katika mwaka wa fedha 2025/2026, serikali inatarajia kukusanya Sh 3.3 trilioni, huku matumizi yakiwa Sh4.29 trilioni. Imetengea maendeleo Sh693.2 bilioni pekee.

Nakisi katika bajeti itajazwa kwa mikopo na kuongeza mzigo wa deni kwa wananchi ambao wanalemewa na gharama ya maisha.

Bajeti hii inalenga kuonyesha kuwa serikali inawajali wananchi. Mfano, zaidi ya Sh702 bilioni zimetengwa kwa elimu ikiwa ni takriban asilimia 28 ya bajeti nzima.

Kadhalika, serikali imetenga Sh138 bilioni kwa sekta ya afya, na ahadi ya kuendeleza Huduma ya Afya kwa Wote (UHC).

Bajeti hiyo iliwaacha hoi wahudumu wa afya walio kwenye mgomo kwa wiki 18 sasa baada ya serikali kuahirisha tena mpango wa kuwaajiri kwa masharti ya kudumu na pensheni hadi mwaka wa fedha unaofuata.

“Nimeongeza mgao wa sekta ya afya hadi Sh138.1 bilioni kutoka Sh123B ili kusaidia shughuli mbalimbali. Upatikanaji wa huduma bora na nafuu kupitia UHC ni kipaumbele cha serikali.”

Serikali imetenga Sh47.6b kwa sekta ya kilimo, Sh128.3b kwa nyumba za bei nafuu, Sh29.7b kwa michezo na Sh300m kwa Hazina ya Hasla ambayo watu wengi wameketaa kurudisha mabilioni waliyokopa.

“Nimependekeza Sh47.6 bilioni kwa sekta ya kilimo, licha ya kuwa sekta hii inapaswa kusimamiwa na serikali za kaunti. Serikali itaongeza msaada kwa wakulima kupitia ufadhili wa pembejeo, ruzuku, na huduma za nyanjani,” alisema.

Kwa Mbadi kusema kuwa Mswada wa Fedha wa 2025 haupendekezi ushuru mpya, wala kuongeza viwango vya sasa ni kutuliza hasira za wananchi waliowahi kuandamana mwaka uliopita kupinga ongezeko la ushuru.

Waziri alisema uchumi umeendelea kuwa imara kwa asilimia 5.2 kwa wastani kati ya 2023 na 2024. Lakini swali ni: huu uchumi unawakilisha nani kwa kuwa mamilioni ya vijana hawana ajira, akina mama nao wanahangaika kupata mlo.

“Nimependekeza Sh3.8 bilioni kwa ajili ya kuwapa makazi wasio na ardhi. Serikali imejitolea kutekeleza mageuzi ya ardhi ili kurekebisha ukosefu wa usawa wa kihistoria, kuhakikisha upatikanaji sawa na usimamizi endelevu wa ardhi,” alisema Bw Mbadi.

Licha ya wafanyakazi kulalamikia ushuru wa nyumba, Bw Mbadi alitengea sekta ya makazi Sh128.3 bilioni.

Katika bajeti hiyo, Bw Mbadi alitenga Sh105.6b kusaidia vijana, wanawake na miradi ya maendeleo mashinani huku akionekana kufurahisha wabunge kwa kutenga Sh58.8b kwa Hazina iliyoharamishwa na korti ya NG-CDF.

Bw Mbadi alitengea Wizara ya Ulinzi Sh202.3b, Sh125.7B kwa Huduma ya Taifa ya Polisi, Sh51.4b kwa Shirika la Kitaifa la Ujasusi( NIS), Sh32.5B kwa usalama wa ndani na utawala wa kitaifa, na Sh38.1b kwa huduma za magereza.

Vile vile alitengea Idara ya mahakama Sh27 bilioni.