Gen Z walivyogeuza mchakato wa kuandaa makadirio ya bajeti
Maandamano ya vijana wa kizazi cha Gen Z nchini dhidi ya Mswada wa Fedha 2024 ulioanzisha ushuru mkubwa yaliyofikia kilele kwa uvamizi bungeni yaliacha athari kubwa kwa mchakato wa kutayarisha bajeti.
Maandamano hayo ya Gen Z, ambayo yalipelekea vifo vya Wakenya zaidi ya 50—wengi wao wakiwa vijana—hayakuwa bure kwani Mswada wa Fedha wa 2024 uliporomoka baada ya Rais William Ruto kukataa kuutia saini kuwa sheria.
Kuporomoka kwa Mswada huo, ambao hutungwa kila mwaka kusaidia kufadhili bajeti ya serikali kuu, kulitokana na pingamizi kwamba ulipendekeza ushuru dhalimu, huku wabunge wakipuuza wito wa Wakenya wafute vifungu walivyokosoa.
Mtaalamu wa masuala ya utawala, Bw Barasa Nyukuri anasema, “angalau juhudi za Gen Z kupinga ushuru wa juu hazikwenda bure.”Bw Nyukuri alibainisha kuwa, utaratibu wa sasa wa utayarishaji wa bajeti ni bora kuliko ule wa awali ambao anasema ulikuwa wa siri.
“Hapo awali, serikali haikujali maoni ya Wakenya kuhusu masuala muhimu ya sera na sheria kama vile ushuru. Maamuzi yalikuwa yakifanywa kwa amri ya watawala.
Lakini tangu mwaka jana, tunaona mabadiliko katika jinsi bajeti inavyotayarishwa,” alisema Bw Nyukuri.Kwa mujibu wa Taasisi ya Masuala ya Kiuchumi (IEA), kizazi cha Gen Z, kwa ustadi wao wa kidijitali na maoni yao makali, kimeathiri kwa kiasi kikubwa utayarishaji wa bajeti na utawala.
“Wameonyesha nguvu za pamoja kupitia mitandao ya kijamii, wakiongoza maamuzi ya sera kama Mswada wa Fedha wa 2024 Kenya. Pia wanajulikana kwa uelewa wao wa kifedha na ujuzi wa kupanga bajeti, mara nyingi wakitumia mitandao ya kijamii kuhamasisha kuhusu uwekaji akiba na matumizi ya busara,” IEA ilieleza katika ripoti yake.
“Kutokuwa na imani kwao na taasisi za jadi na uelewa wao unaoongezeka kuhusu tofauti za kiuchumi kumewafanya watake uwazi na uwajibikaji zaidi katika utawala,” IEA iliongeza.