Habari

Uchunguzi waonyesha wawili waliotekwa Marakwet walinyongwa

Na MERCY KOSKEI June 14th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

UCHUNGUZI wa maiti uliofanywa kwa miili ya wakazi wawili wa Elgeyo Marakwet waliodaiwa kutekwa nyara na maafisa wa polisi kabla ya miili yao kutupwa kando ya barabara katika eneo la Rongai, Kaunti ya Nakuru, umebaini kwamba waliuawa kwa kukabwa koo.

Collins Kipyatich mwenye umri wa miaka 22 na Simeon Yego Chacha, 45, walitoweka mnamo Mei 30 na miili yao ilipatikana Juni 1 na wakazi waliowaarifu polisi.

Uchunguzi wa maiti ulifanywa Alhamisi alasiri katika mochari jijini Nakuru na daktari wa serikali, Dkt Titus Ngulungu, na ulishuhudiwa na familia pamoja na wanaharakati wa haki za binadamu.

Dkt Ngulungu alieleza kuwa Kipyatich alifariki kutokana na kukosa hewa kulikosababishwa na kunyongwa kwa mikono, huku Chacha akifariki kwa kuzibwa mdomo na pua.

Aidha, daktari huyo alisema mikono ya wote wawili ilikuwa imekatwa. Kipyatich alipata majeraha ya misuli, huku mwili wa Chacha ukiwa na majeraha mengi ya kupigwa kwa vifaa butu.

“Kufuatia uchunguzi wangu, niliweza kubaini kwamba chanzo cha vifo vya wote wawili kilikuwa ni kukosa hewa. Tumekusanya sampuli kwa uchunguzi wa kubaini iwapo walikuwa na sumu mwilini,” alisema Dkt Ngulungu.

Akizungumza na wanahabari baada ya kushuhudia uchunguzi wa maiti ya ndugu yake, Bw Benjamin Yego alisema kuwa Chacha aliteswa sana kabla ya kuuawa.

Alieleza kuwa marehemu alikuwa na majeraha kifuani, magoti yaliyovunjika na daktari alithibitisha kuwa alinyimwa hewa hadi kufa.

Pua na mdomo wake vilikuwa vimeharibika na mapafu yake yalikuwa yameporomoka.

“Tutamzika ndugu yetu bila mikono. Tumesikitika sana. Kutoka kwa hali ya miili tuliyoiona, inaonyesha kuwa waliteswa kwa zaidi ya siku mbili. Kama familia tunataka kujua ukweli. Hatuelewi kwa nini aliuawa, alikuwa mfanyabiashara maarufu tu kule Tot,” alisema Bw Yego.

Aliongeza kuwa gari la Chacha aina ya Probox lililoibwa wakati wa utekaji huo lilifuatiliwa hadi Westlands, kisha Ruaka na baadaye Kariobangi kabla ya kutoweka kabisa.

Kwa upande wake, Bw Richard Chebet alisema kuwa mpwa wake Kipyatich alikuwa na alama ya kamba shingoni, ishara kuwa alikabwa koo, na damu iliyoganda sehemu mbalimbali za mwili, ishara kuwa alipigwa.Alifafanua kuwa Kipyatich alichukuliwa kutoka kituo cha afya cha Tot alipokuwa ameenda kutafuta matibabu.

Baba huyo wa watoto wawili alipelekwa katika kituo cha polisi cha Tot lakini baada ya familia kujaribu kumtafuta huko, hawakumpata.

Kulingana na Bw Chebet, Kipyatich hakurekodiwa katika kitabu cha kumbukumbu cha kituo cha polisi licha ya kuchukuliwa na maafisa wa usalama, na juhudi za familia kupata majibu zilizimwa na maafisa waliowafukuza kwa hasira.

“Hatuelewi ni kosa gani alifanya hadi akatendewa hivi. Majeraha ni mengi mno. Ameacha familia changa; mke wake ana mtoto wa wiki mbili tu. Hakuwa mhalifu; alikuwa mkulima anayetambulika. Kama kweli alikosea, wangeweza tu kumkamata na kumpeleka kortini, si kumuua. Na alikuwa mgonjwa walipomchukua,” alisema kwa uchungu.

Mkurugenzi Mkuu wa Muungano wa Watetezi wa Haki za Kibinadamu Nakuru na mwangalizi wa IMLU kanda ya Bonde la Ufa, Bw David Kuria, alitoa wito wa uchunguzi wa haraka kubaini nia halisi ya mauaji hayo.Alisema kuwa marehemu waliteswa sana na huenda waliotekeleza mauaji walikuwa wakitafuta kitu fulani kutoka kwao.