Kenya Divas tayari kwa netiboli ya Milki za Kiarabu
TIMU ya taifa ya mpira wa pete (netiboli) ya wanawake ya Kenya maarufu kama Divas, iliwasili Dubai siku ya Ijumaa kabla ya mechi yao ya ufunguzi dhidi ya timu inayopigiwa upatu, Namibia, kwenye Kombe la Milki za Kiarabu litakaloandaliwa kwa mara ya kwanza kuanzia Jumapili, Juni 15, 2025.
Mashindano hayo, yatakayofanyika Juni 15-21, yatachezwa kwa mfumo wa mzunguko katika ukumbi wa Sheikh Rashid bin Hamdan katika klabu ya Al Nasr.
Wapinzani wa Kenya ni Namibia, Singapore, Milki za Kiarabu, Jamhuri ya Ireland na Amerika.
Rais wa Shirikisho la Netiboli Kenya, Immaculate Kavutha, amesifu timu ya Kenya kushiriki dimba hilo akisema ni hatua kubwa kuelekea kutambulika kimataifa.
“Mashindano haya ni sehemu ya kalenda rasmi ya viwango vya ubora vya dunia. Yanadhihirisha ukuaji wa timu yetu, kujitolea kwao na uungwaji mkono wa kipekee kutoka kwa serikali ya Kenya,” akasema Kavutha.
Timu ya Namibia almaarufu Debmarine Desert Jewels, inaorodheshwa juu kabisa kwenye mashindano haya ikiwa nafasi ya 18 duniani. Kenya inapatikana katika nafasi ya 25, ikiwa imepiga hatua kubwa chini ya kocha kutoka Uganda, Mugisha Ali, ambaye alichukua usukani timu ikiwa nafasi ya 40 duniani.
“Tunalenga kuleta ushindani wa kweli na ari kubwa kwenye mashindano haya ya kipekee. Wachezaji wako katika hali nzuri baada ya maandalizi ya wiki tatu. Lengo letu kuu ni kuboresha nafasi yetu ya dunia,” akasema Ali.
Nahodha Parin Simiyu ana imani kubwa na uwezo wa Divas, akisisitiza juu ya uzoefu unaokuwa wa kimataifa.
“Lengo letu si kushiriki tu, bali pia tunataka kushinda kombe hili na kuimarisha nafasi yetu ya dunia. Divas wapo tayari na wamefanya kazi kwa bidii kufikia malengo yao,” akasema Simiyu.
Mbali na mashindano ya Milki za Kiarabu, Katibu Mkuu wa Shirikisho la Netiboli Kenya, Millicent Busolo, amethibitisha kuwa Divas watashiriki pia mipepetano ya kimataifa nchini Malawi, Zimbabwe na Trinidad & Tobago kama sehemu ya matayarisho ya kuelekea Michezo ya Jumuiya ya Madola ya Glasgow mwaka 2026.