Zaidi ya nguruwe 1,000 waangamizwa na Homa
ZAIDI ya nguruwe 1,000 wamefariki katika Kaunti ya Kiambu kutokana na ugonjwa wa African Swine Fever (ASF), huku Serikali ikiongeza juhudi za kudhibiti kuenea kwa homa hiyo ya nguruwe ambayo imeendelea kusababisha hasara kubwa kwa wafugaji maeneo mbalimbali nchini.
Kurugenzi ya Huduma za Mifugo Nchini, ndiyo Directorate of Veterinary Services (DVS) imeagiza idara za mifugo katika kaunti kuimarisha ufuatiliaji wa magonjwa, usalama wa mashamba, kudhibiti uhamishaji wa nguruwe na kuzindua kikosi cha kukabiliana haraka na milipuko.
Milipuko mikubwa imeripotiwa katika kaunti za Tharaka-Nithi, Kiambu, Busia, Embu, Kakamega, Siaya na Migori, miongoni mwa nyingine, na kusababisha vifo vya nguruwe wengi na hasara za kiuchumi kwa wafugaji.
Mkurugenzi wa Huduma za Mifugo katika Idara ya Maendeleo ya Mifugo chini ya Wizara ya Kilimo na Maendeleo ya Mifugo, Dkt Allan Azegele, alisema ASF ni ugonjwa unaoambukizwa kwa urahisi na kuenea haraka miongoni mwa nguruwe, huku kiwango cha vifo kikifikia asilimia 70 kulingana na aina ya virusi, umri na uwezo wa mnyama kukabiliana na ugonjwa huo. “Nguruwe wakubwa na wadogo wanaweza kuathirika pakubwa,” alisema kwenye mahojiano na ‘Akilimali Dijitali’.
Takwimu za Kenya Animal Biosurveillance System (KABS) na Laboratory Information Management System (LIMS) za Januari hadi Juni 2026 zinaonyesha kuwa ugonjwa huo umeripotiwa katika maeneo kadhaa.
Tharaka-Nithi ilirekodi visa 108 vya maambukizi na vifo 97 kati ya Januari 5 na 11, sawa na kiwango cha vifo cha karibu asilimia 90. Embu ilirekodi visa vitatu na kifo kimoja kati ya Mei 18 na 24.

Hata hivyo, mlipuko mkubwa zaidi umeshuhudiwa Kiambu, ambako zaidi ya mashamba 20 eneo la Juja, Thika na Ruiru yameathirika tangu katikati mwa Mei. Karibu nguruwe 1,470 wameripotiwa kuugua au kufa, huku baadhi ya wafugaji wakipoteza hadi asilimia 100 ya nguruwe.
Kwenye mahojiano Dkt Azegele alithibitisha kuwa ASF haiambukizwi kwa binadamu wala kuwa tishio kwa afya ya umma. “Nyama ya nguruwe iliyokaguliwa na kuthibitishwa na mkaguzi aliyeidhinishwa ni salama kwa matumizi,” alisema.
Hata hivyo, Homa hiyo ya nguruwe inaweza kuangamiza mifugo yote na kuvuruga biashara, kuwaacha wafugaji bila mapato. Hasara za kiuchumi zinazohusishwa na ASF nchini hukadiriwa kufikia Dola 7 milioni (Sh905.1 milioni) kila mwaka.
Kwa sasa hakuna tiba wala chanjo inayopatikana kibiashara dhidi ya aina za virusi vya ASF zinazosambaa nchini. Azegele alisema kukua haraka kwa virusi kunafanya iwe vigumu kutengeneza chanjo inayofaa kwa aina zote.
Aidha, aliwataka wafugaji kuimarisha usalama wa mashamba kwa kudhibiti watu, wanyama, magari na vifaa vinavyoingia katika makao ya nguruwe. “Nguruwe wapya wanapaswa kununuliwa kutoka kwa wazalishaji wanaoaminika, kutengwa na kufuatiliwa kabla ya kuunganishwa na wengine,” alishauri afisa huyo.
Magari yanayoingia na kutoka mashambani yanapaswa kusafishwa kwa dawa, huku sehemu za kuoshea miguu zikiwekwa karibu na makazi ya nguruwe. Wafugaji, pia, wameonywa dhidi ya kuwapa nguruwe mabaki ya chakula ambayo hayajatibiwa.

Dkt Azegele alisema mabaki ya chakula kutoka kwa hoteli yanapaswa kupikwa vizuri kabla ya kupewa nguruwe, huku akisema kupika mabaki hayo kwa kutumia karibu asilimia mbili ya soda ash au magadi soda kunaweza kusaidia kuangamiza virusi.
Serikali pia imewataka wafugaji kuripoti mara moja dalili zisizo za kawaida au vifo vya ghafla vya nguruwe kwa maafisa wa mifugo. Katika maeneo yaliyoathirika, wakulima wanapaswa kufuata masharti ya karantini na udhibiti wa uhamishaji wa wanyama.
Mizoga ya nguruwe inapaswa kutupwa kwa usalama na uangalifu chini ya mwongozo wa maafisa wa mifugo ili kuzuia kuenea zaidi kwa virusi vya Homa ya nguruwe, ASF.
Dkt Azegele alisema idara za mifugo katika kaunti zimeagizwa kuongeza kasi ya ukaguzi katika masoko ya mifugo, machinjioni na maeneo ya kuuza nyama za nguruwe. Hali kadhalika, zitahakikisha visa vinavyoshukiwa vinathibitishwa kwenye maabara kwa haraka, mienendo ya wanyama inafuatiliwa na wafugaji kuelimishwa kuhusu dalili za ugonjwa huo.
Virusi vinavyosambaa nchini ni vya Genotype IX, aina ambayo tafiti zimeonyesha kuwa na uwezo mkubwa wa kusababisha maradhi mbaya na vifo vingi.

Wasiwasi zaidi umeibuliwa na uwepo wa nguruwe wanaobeba virusi bila kuonyesha dalili. Utafiti ulibaini virusi vya ASF katika tishu za viungo vya ndani vya asilimia 15.9 ya nguruwe walioonekana kuwa na afya katika eneo la mpaka wa Kenya na Uganda.
Serikali imezindua mfumo wa kidijitali kusajili mifugo nchini unaojulikana kama Animal Identification and Traceability System (ANITRAC), utakaosaidia kutambua wanyama na wamiliki wao, pamoja na kufuatilia historia yao, magonjwa na mienendo tangu kuzaliwa hadi kuchinjwa, kusafirishwa nje au kufariki.
Kwa sasa, asasi mbalimbali za mifugo zimeagizwa kuimarisha ufuatiliaji katika maeneo yaliyo katika hatari kubwa, hasa Kiambu, Tharaka-Nithi na Embu, pamoja na maeneo ya mipakani. Kenya inakadiriwa kuwa na takriban nguruwe 800,000.