KINAYA: Miti ya kisiasa inateleza, nao nyani wanaanguka kiholela!
SIKU ya kufa kwa nyani miti yote huteleza. Sijui kwa nini napenda sana kuwaona nyani wakiteleza mitini na kuanguka pu! Kufa kwao sijutii, nashabikia.
Wakati mwingine mimi hujiuliza: Baada ya nyani huyo kufa, mwingine atakayefuata ni nani?
Hata kabla sijajijibu, wanaanguka wengi, shughuli nzima inageuka starehe ya kuketi kitako kujionea wakianguka na kufa.
Katika muktadha wa siasa za Kenya, nyani tayari wameanza kuteleza, na wanaanguka. Licha ya ujanja wao wote wameshindwa kujishikilia mitini. Ajabu!
Je, unakumbuka Mbunge wa Gatundu Kaskazini, Gabriel Kagombe, aliyekuwa mtetezi wa Kasongo? Inaonekana amevunjikia mguu malishoni na sasa amerejea zizini kusaidiwa.
Je, unakumbuka Mbunge Mwakilishi wa Kike Lamu, Monicah Marubu Muthoni, enzi akitumia kipaza sauti kujaribu kuwanyamazisha wasiompenda Kasongo? Huyo pia amemtoroka na kuingia upinzani.
Nakuhakikishia kuwa wengine wengi watahama kutoka serikalini wakitoa visingizio vya ajabu kwa nini wanaamini Kasongo na Kenya Kwanza yake hawafai kuongoza nchi.
Hata kabla hujaanza kusherehekea kuhama huko, na labda kuona taswira ya nyani akianguka kutoka mtini, jiulize nyani anayeanguka ni nani hapa.
Je, ni Kasongo au hao wanaomtoroka? Labda ni wote wawili, Kasongo na watoro hao?
Wengi wanaojiondoa serikalini wakati huu, hasa wanaotokea mlimani au walio na asili ya huko, wanadhani hatugundui ujanja wao. Wajinga waliisha Kenya!
Wamejua kwamba kwao Kasongo ni sawa na nyama ya nguruwe Saudia, hainunuliki hata ukiinadi namna gani.
Ndiposa wanamtoroka ili waweze kuchaguliwa, kisha warudiane naye. Ujanja wa ndoa ya kisiasa eti.
Jiulize hivi, wakimtoroka Kasongo wanamnyima kura ngapi? Kumtoroka kutasababisha ashindwe uchaguzini?
Wamemtoroka ili wajinusuru kisiasa kwani kimbunga kinachofagia wafuasi wa Kasongo huko Mlimani hakimsazi yeyote.
Pale Mlimani kumla nguruwe ni haramu, na kila atakayethubutu atajikaanga kwa mafuta yake mwenyewe kama ilivyo kawaida ya hayawani huyo.
Swali kuu linaloibuka kila tunaposikia mtu amemtoroka Kasongo ni, kwa nini wakati huu? Labda baada ya kushiba minofu ya Kenya Kwanza? Mifupa ya kwetu wataiweza?
Hivi wanadhani mpigakura ana akili za ngiri, yaani za kusahau tabia na mienendo yao?
Utaona maajabu kati ya sasa na uchaguzi mkuu ujao. Watu watasalitiana, kisa na maana kuchaguliwa.
Kwa kuogopa kuanguka kama nyani, wengi watatoa visingizo vya kubadili misimamo ya kisiasa, hata wamtoroke Kasongo.
Usidanganyike. Kumbuka tabia za kinyonga ni zile zile za kubadili rangi kutegemea mazingira aliyomo.
Nyani wa kuanguka na waanguke kishenzi! Miti na iteleze kabisa!
– Douglas Mutua ni mwanahabari Mkenya anayeishi Amerika (mutua_muema@yahoo.com)