Ruku ataka vijana wakumbatie mafunzo ya kiufundi ili wajiajiri
WAZIRI wa Utumishi wa Umma Geoffrey Ruku amewataka vijana wakumbatie mafunzo ya serikali ambayo yanalenga kuwapa ujuzi wa kiufundi ili wawahi nafasi za ajira na hata kujiajiri.
Bw Ruku alisisitiza umuhimu wa kujiendeleza kiujuzi ili kupambana na ukosefu wa ajira na kijiinua kiuchumi. Pia alisifu serikali kwa kulenga kuwapa mafunzo na ujuzi vijana kupitia Vyuo vya Mafunzo ya Kiufundi (TVET) akisema hilo litawatayarisha kwa kazi zinazokuja.
Waziri huyo alikuwa akiongea wakati wa kutoa basi kwa Taasisi ya Mafunzo ya Kiufundi ya Chuka Igamba Ng’ombe, Kaunti ya Tharaka-Nithi.
Basi hilo litakuwa likitumika kuwasafirisha wanafunzi wakitembelea maeneo mbalimbali ili kupata mafunzo.
Wakati wa hafla hiyo, Bw Ruku alitangaza kuwa serikali inalenga kujenga nyumba 1750 katika TVET ya Chuka ili kuwapa hifadhi zaidi ya wanafunzi 4,300.
Kwenye hotuba yake, waziri huyo alitetea uongozi wa Kenya Kwanza akisema umeanza kufufua miradi ambayo ilikuwa imekwama hapo awali.
Baadhi ya miradi aliyoitaja ni Hospitali ya Natasha Memorial kwa kima cha Sh200 milioni kule Kibugua, soko la kisasa kwa kima cha Sh300 milioni mjini Chuka na masoko mengine ya Chera na Kanjuki ambazo zimegharimu Sh56 milioni kila moja.
Bw Ruku alikuwa ameandamana na wabunge Patrick Munene (Chuka/Igamba Ngómbe), Mbunge Mteule Sabina Chege, Mugambi Rindikiri (Buuri) na Gabriel Kagombe (Gatundu Kusini).
Wanasiasa hao walitumia muda huo kukashifu wapinzani wa Rais William Ruto wakisema mrengo huo hauna chochote cha kuwafaa wakazi wa eneo hilo.