Kampuni yalenga nishati ya jua kulinda mazingira
Kampuni ya Tata Chemicals Magadi Limited (TCML), iliyoko katika Kaunti ya Kajiado, imeanza mradi mkubwa wa kutumia nishati safi mbadala ya mafuta ili kupunguza gharama ya uzalishaji na kuimarisha uendelevu wa mazingira.
Kampuni hiyo imetayarisha mipango ya kina ya kuongeza zaidi ya mara mbili uzalishaji wa umeme wa nishati mbadala katika kipindi cha miaka mitano ijayo.
Mradi huu mkubwa wa kuzalisha nishati ya jua utatekelezwa kwa awamu mbili na unatarajiwa kuzalisha megawati 10 baada ya kukamilika. Awamu ya kwanza inayozalisha megawati tano itazinduliwa mwezi Julai. Uunganishaji wa awamu ya pili ya megawati tano utaanza mara baada ya awamu ya kwanza kuzinduliwa.
Mitambo ya sola inawekwa katika kipande cha ardhi cha ekari tano ndani ya eneo kubwa linalomilikiwa na kampuni hiyo huko Magadi, katika Tarafa ya Kajiado Magharibi.
Steve Okiri, Mkuu wa Biashara alisema kuwa kampuni hiyo kwa sasa iko katika mchakato wa kubadilika kutoka matumizi ya mafuta hadi nishati safi kwa lengo la kulinda mazingira.
“Kampuni pia imepunguza matumizi yake ya umeme kutoka megawati 35,227 mwaka wa 2023 hadi 30,676 mwaka wa 2024,” alisema Bw Okiri.
Wenyeji wamehusishwa katika ujenzi wa mradi huu mkubwa wa kupokea nishati ya jua, ikizingatiwa kuwa eneo la Magadi hupokea jua kali na joto la kupindukia kwa muda mrefu.
Kampuni hiyo inalenga kupunguza kutegemea gridi ya kitaifa na hivyo kupunguza kwa kiasi kikubwa gharama ya uzalishaji.
Meneja katika kampuni hiyo Bw Joseph Kombo, alisema kuwa mradi huo ulikumbana na changamoto nyingi katika hatua ya mwanzo lakini sasa awamu ya kwanza iko karibu kukamilika kwa asilimia 95.