Afisa wa Umma kulipwa fidia ya Sh3.3 milioni kwa kuharibiwa jina mitandaoni
MAHAKAMA mmoja ya Siaya imemwamuru mwanamume mmoja kulipa fidia ya Sh3.3 milioni kwa kumchafulia jina afisa mmoja wa umma kwenye majukwaa ya mitandao ya Facebook na WhatsApp.
Katika kesi hiyo, Afisa Mkuu Mtendaji wa Bodi ya Utumishi wa Umma, Kaunti ya Siaya Wilfred Ouma Nyagudi alimshtaki Michael Ochieng’ almaarufu Mike Ochieng’ kwa kusambaza taarifa za kumharibia sifa, zikiandamanishwa na picha zake, kwenye mitandao ya kijamii.
Hakimu Jacob Mkala aliamua kwamba Bw Nyagudi aliathirika kwa kuharibiwa jina kutokana na jumbe hizo ambazo kwanza ziliwekwa kwenye Facebook na baadaye kusambazwa katika makundi kadhaa ya WhatsApp katika Kaunti ya Siaya.
Mshtakiwa atamlipa mlalamishi Sh3 milioni kwa kumharibia jina na Sh300,000 kwa kusambaza picha zake kwenye mtandao ya kijamii bila idhini yake.
Mahakama pia aliagiza Bw Ochieng kufuta kabisa jumbe hizo zote kutoka mitandao ya kijamii na aombe msamaha kupitia majukwaa hayo.
“Mshtakiwa atafuta jumbe hizo za mbovu kutoka Facebook na WhatsApp na kuomba msamaha bila masharti yoyote kwa mlalamishi,” Hakimu Mkala akasema.
Kesi hiyo iliwasilishwa mahakamani baada ya Bw Ochieng kusambaza picha ya Bw Nyagudi akiindamanisha na maelezo: “Tumwombee Afisa Mkuu Mtendaji wa Bodi ya Utumishi wa Umma, Kaunti ya Siaya Bw Wilfred Nyagudi Jumapili hii ya Matawi….”
Bw Nyagudi alisema taarifa hiyo ililenga kumdhihaki na kulenga kumsawiri vibaya haswa inapoandamanishwa na picha yake.
Alieleza kuwa maneno hayo, kimsingi, yaliashiria kuwa yeye ni mfisadi na hafai kushikilia afisi ya umma.
“Maneno hayo kwa kuzingatia maana yao ya kawaida yanalenga kuhakikisha kuwa jamii inanisawiri katika mtu asiye mwadilifu,” Bw Nyagudi akasema kwenye hatikiapo yake.
Aliambia mahakama kwamba jumbe hizo ziliboronga hadhi yake kitaaluma na kuhujumu imani ya umma kwa uongozi wake.