Habari Mseto

Cherargei amshtaki Gachagua NCIC kwa ‘uchochezi’

Na CECIL ODONGO July 28th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

SENETA wa Nandi Samson Cherargei ameandikia Tume ya Kitaifa ya Uwiano na Utangamano (NCIC) barua ya malalamishi akiitaka imchunguze Kiongozi wa DCP, Rigathi Gachagua, kwa madai ya kutoa matamshi yanayoweza kuchochea vurugu za kikabila.

Katika barua ya Julai 27, 2026, iliyonakiliwa kwa Mwenyekiti wa NCIC, Bw Cherargei alisema matamshi ya Bw Gachagua kuhusu jamii ya Wakalenjin yanastahili kuchunguzwa kwa mujibu wa Katiba na Sheria ya Uwiano na Utangamano wa Kitaifa.

Bw Cherargei anadai kuwa kauli hizo, zilizotolewa katika mikutano ya kisiasa na mahojiano ya vyombo vya habari, zimeibua hofu kuhusu athari zake kwa umoja wa kitaifa.

Kulingana na malalamishi hayo, Bw Gachagua anadaiwa kuhusisha baadhi ya wanajamii wa Wakalenjin na uhalifu, ukosefu wa usalama na ghasia zilizopangwa mbali na kutamka matamshi ya chuki.

Seneta huyo alisema aliambatanisha ushahidi baadhi yazo ikiwa ni video na nakala ya hotuba ya Bw Gachagua kufuatia madai ya kutekwa nyara kwa mbunge mmoja.

Anadai kuwa Bw Gachagua alidai baadhi ya maafisa wa serikali kutoka jamii ya Wakalenjin waliunda kikosi maalumu cha polisi cha kuwafuatilia viongozi wa upinzani, madai ambayo hayajathibitishwa na NCIC wala mahakama.