Makala

Mwanamke atafuta usaidizi baada ya kupokonywa mtoto na mpenziwe raia wa Urusi

Na SIAGO CECE June 18th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

MWANAMKE katika Kaunti ya Kwale, analilia haki akidai kuwa, mpenzi wake ambaye ni raia wa Urusi alimpokonya mtoto.

Bi Faith Jerop, alipoombwa na mpenzi wake kutoka Urusi wasafiri kwenda jijini Moscow, alihisi furaha na hofu kwa wakati mmoja.

Alifurahi kuwa atakutana na familia ya mpenzi wake, lakini pia aliingiwa na wasiwasi kuhusu uamuzi huo.

“Aliniambia baba yake anaugua sana na anatamani amwachie mtoto wetu urithi wake kabla hajafa. Licha ya mamangu kunikataza, nilikubali nikijua kuwa tutarudi nyumbani na mtoto,” alisema Bi Jerop, 23.

Waliposafiri kwenda Moscow, alipigwa na butwaa kupelekwa kwenye nyumba ya kupanga, kinyume na alivyoahidiwa kuwa ataenda nyumbani kwao.

Pia alishangaa alipoambiwa alale sebuleni wala si katika chumba cha kulala.

Bi Jerop na mpenzi wake walikutana miaka miwili iliyopita katika mji wa kitalii wa Diani, Kaunti ya Kwale. Baada ya miezi mitatu, Bi Jerop alikuwa mjamzito.

“Nilipomwambia niko mjamzito, alitaka nitoe mimba. Lakini mama yangu alikataa,” alieleza.

Baadaye, raia huyo wa Urusi alimwambia atafute pasipoti ya usafiri waende Argentina ili aweze kujifungulia huko, lakini pasipoti ilichelewa na mtalii huyo akarudi peke yake.

Alirudi nchini Kenya tena baada ya miezi kadhaa na kuishi na familia ya Bi Jerop kwa miezi sita.

“Aliishi kwetu Diani, akimwangalia mtoto tu. Akaanza kutengeneza vyeti vya kuzaliwa na pasipoti yetu,” alisema Bi Jerop.

Mtoto alipotimiza mwaka mmoja, waliondoka kwenda Urusi. Licha ya Bi Jerop kuonywa na mamake, aliamua kumfuata mpenzi wake baada ya kuambiwa tayari tiketi zilishanunuliwa za Aprili 11, mwaka huu.

Mwezi mmoja baadaye, Bi Jerop alirudi nchini, bila mtoto wake wa mwaka mmoja. Familia hiyo sasa imeomba serikali kuingilia kati suala hilo ikisema kuwa ingetaka kumwona mwanao tena.

“Ninahisi kusikitika sana. Mwezi mmoja sasa umeisha bila kumwona mtoto wangu na nina wasiwasi kuhusu hali yake. Hata hivyo sitakata tamaa ya kumtafuta mtoto wangu,” Bi Jerop alisema.

Aliongeza kuwa, mwanamume huyo mwenye umri wa miaka 41 alibaki na mtoto wake, kinyume na sheria au makubaliano yeyote.

Bi Jeniffer Ekitela, ambaye ni mamake Bi Jerop, alieleza kuwa familia hiyo imekumbwa na huzuni, akitaka Wizara ya Mashauri ya Kigeni na serikali ya kaunti kuisadia.

“Nilikuwa na hisia mbaya kuhusu mahusiano ya mwanngu na mtalii huo na nilimwambia kila mara. Lakini sasa tuko katika hali hii na ningependa kumwona mjukuu wangu tena,” Bi Ekitela alisema.

Kwa sasa, familia hiyo imeanza mchango wa kumsaidia Bi Jerop kupata wakili atakayemsaidia kuanzisha kesi ya kurudishiwa mwanawe.