UAMUZI wa Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna kupinga mahakamani hatua ya ODM kumuondoa katika wadhifa wa Katibu Mkuu, unatazamwa na wachanganuzi wa siasa kama mkakati wa kumpa muda, kulinda ushawishi wake na kuacha milango wazi kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.

Badala ya kukubali uamuzi wa chama na kuondoka kimya kimya, Sifuna ameanzisha vita vya kisheria vinavyoweza kuchukua miezi kadhaa, na hivyo kuendeleza mjadala kuhusu hatima yake kisiasa huku akiendelea kujitambulisha kama mmoja wa viongozi wakuu wa ODM na upinzani.

Mgogoro huo uliongezeka wiki hii baada ya Kamati Kuu ya Kitaifa (NEC) ya ODM kupitisha mapendekezo ya Kamati ya Ndani ya Kutatua Migogoro (IDRC) ya kumuondoa Sifuna kama Katibu Mkuu.

Kaimu Katibu Mkuu Catherine Omanyo alisema NEC ilikubaliana na mapendekezo hayo baada ya kupitia ripoti ya kamati hiyo, ikisisitiza kuwa mchakato huo ulifuata katiba ya chama.

ODM inamlaumu Sifuna kwa kupinga hadharani misimamo rasmi ya chama, kukosoa makubaliano ya ushirikiano kati ya ODM na UDA ya Rais William Ruto, kushiriki shughuli za kisiasa bila idhini na kukosa kuhudhuria mikutano muhimu ya chama.

Chanzo kikuu cha mzozo huo ni msimamo wa Sifuna kwamba mkataba wa ushirikiano kati ya ODM na UDA umekufa kisiasa, kauli ambayo imekuwa ikipingana na viongozi wa juu wa chama wanaouunga mkono.

Lakini wachambuzi wanasema mapambano ya mahakamani huenda si kuhusu ushindi wa kisheria pekee bali ni mbinu ya kisiasa.

Mchambuzi wa siasa Arnold Maliba anasema kesi hiyo inampa Sifuna nafasi ya kuendelea kuonekana kwenye ulingo wa kisiasa huku ODM ikilazimika kujitetea mbele ya umma.

‘Kadri kesi inavyoendelea, ndivyo Sifuna anavyoendelea kujenga ushawishi wake. Hizi si vita vya mahakamani pekee bali ni vita vya uhalali wa kisiasa na kuungwa mkono na wananchi,’ alisema.

Mchambuzi mwingine, Rachael Omollo, anasema kesi za kisiasa nchini mara nyingi huchukua muda mrefu, jambo linalompa Sifuna nafasi ya kuendelea kushikilia ushawishi wake huku akijionyesha kama mwathiriwa wa migogoro ya ndani ya chama.

Kwa mujibu wake, hatua ya kukimbia mahakamani pia inampa fursa ya kuelekeza mjadala wa kisiasa kwa manufaa yake na kuchelewesha utekelezaji wa adhabu dhidi yake.

Wafuasi wa Sifuna wanasema suala hilo linahusu zaidi demokrasia ndani ya vyama vya siasa na uhuru wa viongozi kutoa maoni tofauti bila kuadhibiwa.

Miongoni mwa wanaomtetea ni Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi, ambaye pia aliwahi kuondolewa katika nafasi ya Naibu Kiongozi wa Chama cha ODM.

Osotsi anadai mchakato uliotumika kumuondoa Sifuna ulikuwa na dosari nyingi na haukumpa nafasi ya haki ya kujitetea.

Anasema kamati ya kushughulikia migogoro ilikuwa na upendeleo tangu mwanzo na kwamba NEC iliharakisha kupitisha mapendekezo hayo licha ya masuala ya kisheria yaliyoibuliwa awali.

Hata hivyo, viongozi wa ODM wamekanusha madai hayo.

Mbunge wa Rarieda Otiende Amollo amesema Sifuna alipewa nafasi ya kujibu tuhuma zote kupitia wakili wake Isaack Okero, hivyo haki ya kusikilizwa ilizingatiwa.

ODM inasisitiza kuwa hakuna kiongozi aliye juu ya katiba ya chama na hatua za kinidhamu zinalenga kulinda umoja na nidhamu, si kunyanyasa viongozi wenye maoni tofauti.

Kwa upande wake, wakili Chris Omore anaamini kesi hiyo inampa Sifuna nafasi ya kuimarisha uhusiano wake na viongozi wengine wa upinzani huku akiamua ikiwa ataendelea kubaki ODM au atachukua mkondo mwingine wa kisiasa.

Mchambuzi Dismas Mokua naye anasema vita vya mahakamani vinamwezesha Sifuna kubaki ndani ya ODM bila kulazimika kufanya maamuzi ya haraka ambayo yanaweza kuhatarisha kiti chake cha useneta.

Anasema hatua hiyo pia inampa chaguzi tatu: kupatana na viongozi wa ODM, kuongoza vuguvugu la upinzani ndani ya chama au kujadiliana kisiasa kupitia mahakama na mazungumzo.

Katika miezi ya hivi majuzi, Sifuna amekuwa mmoja wa wakosoaji wakubwa wa ushirikiano kati ya ODM na serikali ya Kenya Kwanza.

Kupitia vuguvugu la Linda Mwananchi, amevutia viongozi na vijana wanaopinga ushirikiano huo.

Kwa mujibu wa wachambuzi, kadri mgogoro huo unavyoendelea ndivyo Sifuna anavyoendelea kutawala mijadala ya kisiasa na kujiimarisha mbele ya wafuasi wake. Wanasema huenda hiyo ndiyo sababu amechagua mahakama badala ya kuondoka kimya kimya ndani ya ODM.