Habari

Mapuuza ya wakuu yalivyopalilia ukatili wa polisi dhidi ya raia

Na STEVE OTIENO June 19th, 2025 Kusoma ni dakika: 1

LICHA ya matumaini makuu Wakenya walikuwa nayo kwao, wakuu wa usalama wamekuwa wenye kiburi huku wakikaidi sheria, polisi wakiendelea kushutumiwa kwa mauaji nchini.

Kwa miezi 10 sasa, Inspekta Jenerali wa Polisi Douglas Kanja na Manaibu wake Gilbert Masengeli (Huduma za utawala) na Eliud Lagat (Idara ya polisi) wameonyesha kiburi na mapuuza ambayo yanazua masuali iwapo wanamakinikia utekelezaji wa sheria.

Bw Kanja aliapishwa mnamo Septemba 2024 na kulikuwa na matumaini angeinua hadhi ya idara ya polisi kwa kuyarekebisha maovu yaliyotokea awali.

Akiingia madarakani, kulikuwa na utovu wa usalama mijini na umma ulianza kupoteza imani na utendakazi wa idara ya polisi.

Kinaya ni kuwa, miezi michache baada ya kuingia madarakani hali imekuwa mbaya zaidi huku maisha yakiendelea kupotea mikononi mwa polisi.

Mapema 2025, Mahakama ilimwaagiza afike mbele yake kutoa ufafanuzi kuhusu kutekwa nyara kwa wanaume saba mnamo 2024.

Bw Kanja hakujitokeza hata baada ya amri kadhaa kutolewa, akamulikwa na vyombo vya habari na hata kuonywa kuhusu adhabu ya kukaidi korti. Mara nyingi alikuwa akiwatuma tu wadogo wake kumwakilisha kortini.

Hata Jaji Bahati Mwamuye alitoa onyo la mwisho kwa Bw Kanja na Mkuu wa Idara ya Upelelezi Nchini (DCI) Mohamed Amin na kuonya adhabu kali ya kisheria ingewaangukia, wasingefika.

Wawili hao walikaidi onyo hilo na kupuuza amri ya korti.

Baadaye 2024, Bw Masengeli pia alijipata pabaya kwa kupuuza amri za korti.

Mnamo Septemba mwaka huo, alipatikana na hatia kwa kukosa kufika kortini kueleza walikokuwa mwanaharakati Bob Njagi na ndugu Jamil na Aslam Longton ambao walikuwa wakizuiliwa na polisi chini ya amri yake.

Bw Masengeli alihukumiwa miezi sita gerezani lakini hukumu hiyo haikutekelezwa kwa sababu hakukamatwa na aliendelea kuhudhuria shughuli za umma akitekeleza majukumu yake.