Habari

Waiguru aweka kando ukuruba wake na Ruto, aishambulia serikali

Na GEORGE MUNENE June 20th, 2025 Kusoma ni dakika: 1

GAVANA wa Kirinyaga, Anne Waiguru, Alhamisi alivunja kimya chake na kulaani vikali visa vya utekaji nyara na mauaji ya kiholela vinavyoendelea nchini, katika matamshi yaliyowashangaza wengi kutokana na uhusiano wake wa karibu na Rais William Ruto.

Akizungumza katika Chuo cha Mafunzo ya Ufundi cha Kamiigua kilichoko eneobunge la Gichugu, ambapo alikuwa akikabidhi mitungi ya gesi na matangi ya maji kwa vikundi, Bi Waiguru alisema hali ya sasa ni ya kusikitisha na haikubaliki katika taifa la kidemokrasia.

“Nataka niseme wazi, ni jambo la kusikitisha kwamba katika enzi hizi tunazoishi, katika jamhuri ya kidemokrasia, watu bado wanatekwa nyara, kufungwa kwenye vituo vya polisi na kuuawa huku maafisa wa serikali wakilaumiana badala ya kuwajibika,” alisema Waiguru.

Alisisitiza kwamba wote waliohusika na vitendo vya uhalifu vinavyoacha familia nyingi katika huzuni na majonzi wanapaswa kukamatwa na kufikishwa mahakamani.

“Hatua lazima zichukuliwe,” alisisitiza huku akishangiliwa na hadhira.

Waiguru aliwataka viongozi kuwa na uvumilivu  kisiasa.

“Sisi tunatukanwa kila siku na wapinzani wetu lakini hatuwateki nyara. Kiongozi anayekosa kuvumilia hakustahili kuwa kiongozi,” alisema.

Alionya kuwa ikiwa visa hivyo vitaendelea, Kenya itakuwa katika hatari ya kuyumbishwa na vurugu.

“Hakuna kiongozi mwenye akili timamu anayeweza kuunga mkono utekaji na mauaji ya vijana wetu,” alisema.

Akitaja mauaji ya Albert Ojwang na kisa cha mfanyabiashara wa barakoa aliyepigwa risasi kichwani na polisi, Waiguru alisema visa hivyo vimeitikisa nchi nzima.

“Niliangalia video ya yule mchuuzi wa barakoa, sikuona akimkera afisa wa polisi. Polisi aliyempiga risasi lazima awajibishwe,” aliongeza.

Aliwataka wakazi wa Kirinyaga kuwa wavumilivu akiahidi kuwa atawaelekeza kisiasa kuelekea uchaguzi wa 2027.

“Ninasikiliza sauti za watu kabla ya kutangaza mwelekeo wa kisiasa,” alisema.

Waiguru pia alimshambulia aliyekuwa Naibu Rais, Rigathi Gachagua, akimlaumu kwa kujaribu kumharibia jina katika eneo hilo.

“Amezunguka akisema sijafanya chochote Kirinyaga, lakini maendeleo yangu yanaonekana wazi. Aache kusema uongo,” alisema.