LICHA ya Serikali ya Kaunti ya Mombasa kupiga marufuku uuzaji na matumizi ya muguka miaka miwili iliyopita, utafiti mpya umeonyesha kuwa mmea huo bado ni miongoni mwa dawa zinazotumiwa zaidi na vijana katika kaunti hiyo huku idadi ya watumiaji wa dawa za kulevya nchini ikiongezeka hadi milioni 4.7.

Takwimu za serikali zinaonyesha kuwa Wakenya milioni 4.7 wenye umri wa kati ya miaka 15 na 65 wanatumia angalau aina moja ya dawa za kulevya au mihadarati, ikilinganishwa na takriban milioni 4.2 waliorekodiwa katika tafiti zilizopita.

Akizungumza Mombasa wakati wa maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Kupambana na Matumizi na Biashara Haramu ya Dawa za Kulevya, Katibu katika Wizara ya Usalama wa Ndani, Dkt Raymond Omollo, alisema ongezeko hilo linaonyesha kuwa vita dhidi ya mihadarati bado vina changamoto nyingi.

Alisema serikali imeanza kutumia mbinu mpya za kijasusi na teknolojia kukabiliana na mitandao ya wasafirishaji wa dawa za kulevya, hasa dawa za kisasa zinazotengenezwa kwa kemikali.

‘Mabadiliko katika mbinu zinazotumiwa na wasafirishaji wa dawa yanahitaji mikakati mipya. Serikali imeimarisha ujasusi, ufuatiliaji na ushirikiano kati ya taasisi mbalimbali ili kuhakikisha wahusika wanakamatwa na kufikishwa mahakamani,’ alisema Dkt Omollo.

Naye Gavana wa Mombasa, Abdulswamad Shariff Nassir, alisema utafiti uliofanywa na kaunti hiyo kwa vijana 12,852 uligundua kuwa asilimia 25.7 walikiri kutumia dawa za kulevya, huku matumizi ya sigara, muguka na miraa yakiongezeka.

Matokeo hayo yameibua maswali kuhusu ufanisi wa marufuku ya muguka iliyowekwa na serikali ya kaunti mwaka 2024 kwa lengo la kulinda afya ya vijana.Bw Nassir alisema sheria pekee haitoshi kumaliza tatizo hilo, akisisitiza haja ya kuimarisha elimu kwa umma, ushauri nasaha na huduma za ukarabati kwa waathiriwa wa uraibu.

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Kitaifa ya Kupambana na Pombe na Dawa za Kulevya (NACADA), Dkt Anthony Omerikwa, alisema kaunti 11 tayari zimeanza mchakato wa kuanzisha vituo vya ukarabati ili kusaidia waathiriwa wa dawa za kulevya.

Maafisa wa serikali walisema ongezeko la watumiaji kutoka milioni 4.2 hadi milioni 4.7 linaonyesha kuwa matumizi ya dawa za kulevya sasa ni tatizo la kitaifa linalohitaji ushirikiano wa familia, shule, taasisi za kidini na serikali ili kulinusuru taifa dhidi ya athari zake.