Jamvi La Siasa

2027: Joho, Nassir kupambana na Jicho Pevu mbio za 2027

Na ANTHONY KITIMO June 21st, 2026 Kusoma ni dakika: 2

 JOTO la kisiasa limeanza kupanda katika Kaunti ya Mombasa huku vita vya kuwania kiti cha ugavana mwaka wa 2027 vikianza kuchukua sura mpya, hali inayoweka Mbunge wa Nyali Mohamed Ali maarufu kama Jicho Pevu katika mchuano mkali dhidi ya viongozi wenye ushawishi mkubwa katika eneo la Pwani.
Bw Ali, ambaye amebakia kuwa sauti ya kipekee kisiasa Mombasa, anajitayarisha kufanya jaribio jipya la kutwaa uongozi wa kaunti hiyo katika uchaguzi mkuu wa 2027. Kinyang’anyiro hicho kinatarajiwa kuwa mtihani mkubwa kwa chama cha Orange Democratic Movement (ODM) ambacho kimekuwa kikitawala siasa za Mombasa kwa muda mrefu.
Mbunge huyo wa Nyali, anayetarajiwa kuwania ugavana kupitia chama cha Wiper Democratic Movement, atakutana na upinzani mkali kutoka kwa Waziri wa Madini na Uchumi wa Bahari Hassan Joho na gavana wa sasa Abdulswamad Nassir.
Viongozi wengine kadhaa waliochaguliwa katika kaunti hiyo pia wanahusishwa na mbio hizo, jambo linalofanya kinyang’anyiro hicho kuwa miongoni mwa vyenye ushindani mkubwa zaidi katika eneo la Pwani.
Hatua ya Bw Ali inajiri wakati viongozi wa ODM wanatafuta kuthibitisha kuwa Mombasa bado ni ngome ya chama hicho licha ya mabadiliko ya kisiasa yanayoendelea nchini na ushirikiano unaozidi kuimarika kati ya baadhi ya viongozi wa upinzani na Rais William Ruto.
Akizungumza hivi karibuni, Bw Joho alisisitiza kuwa ODM itaendelea kutawala eneo la Pwani
“Tunaamini Mombasa na eneo lote la Pwani bado ni ngome za ODM. Kuhusu urais tuko pamoja na Rais William Ruto, lakini katika nafasi nyingine tutahakikisha ODM inasalia madarakani kote katika eneo hili,” alisema Bw Joho.
Kwa upande wake, Bw Ali anaona uchaguzi wa 2027 kama nafasi ya kurejelea mkakati uliomwezesha kuishinda mashine ya ODM katika chaguzi zilizopita.
Mbunge huyo amejijengea jina kupitia vita dhidi ya ufisadi, uwazi katika uongozi na msimamo wa kisiasa usioegemea upande wa viongozi wakuu.
Amekuwa mmoja wa viongozi wachache waliochaguliwa Mombasa ambao wameendelea kufuata mkondo wao wa kisiasa, huku gavana, seneta na wabunge wengi wa kaunti hiyo wakijiunga na viongozi wanaounga mkono serikali ya Rais Ruto.
Bw Ali amekuwa akikosoa kile anachokiita vita vya kuchagua dhidi ya ufisadi na kuwatuhumu viongozi wengine kwa kuweka mbele maslahi yao ya kisiasa badala ya kuwahudumia wananchi.
“Simba hawaendi pamoja na kondoo. Ninafuata njia yangu mwenyewe ambayo naamini inalenga maslahi ya wananchi na si kuwa mtumwa wa mwanasiasa fulani,” alisema Bw Ali.