Dkt Nancy Macharia angukia cheo kingine baada ya kustaafu
MAJUMA machache baada ya kustaafu kama Afisa Mkuu Mtendaji wa Tume ya Huduma kwa Walimu (TSC) Nancy Macharia anaelekea kurejea katika utumishi wa umma baada ya kupendekezwa kuwa mwenyekiti wa Bodi ya Utumishi wa Umma katika Kaunti ya Murang’a.
Katika taarifa iliyotolewa Juni 18, 2025 na kutumwa kwa Bunge la Kaunti ya Murang’a, Gavana Irungu Kang’ata amependekeza Dk Macharia kushikilia wadhifa huo endapo madiwani wa kaunti hiyo watamwidhinisha.
“Kwa mujibu wa Sehemu ya 6 ya Sheria ya Uteuzi wa Umma (ya Mabunge ya Kaunti) ya 2017 na Sehemu ya 58A (7) ya Sheria za Serikali ya Kaunti ya 2012, Bunge la Kaunti lilipokea notisi kwamba Gavana wa Murang’a Dkt Irungu Kang’ata amemteua wafuatao kuwa Mwenyekiti, Mwanachama na Katiba wa Bodi ya Utumishi wa Umma, Kaunti ya Murang’a,” ikasema taarifa hiyo iliyowasilishwa kwa bunge.
Wateule hao ni; Dkt Nancy Njeri Macharia (Mwenyekiti), Dkt Louis Mwende Musikali (Mwanachama), Johnson Kang’ethe Kinyua (Mwanachama) na Dkt Brian Lichenga Makamu (Mwanachama).
Naye Bw Oscar Kimani Gathura amependekezwa kuwa Katibu wa bodi hiyo.
Majina hayo yamewasilishwa kwa Kamati ya Utawala, Leba na Masilahi ya Kijamii na Haki na Masuala ya Kisheria itakayowapiga msasa Dkt Macharia na wengine wanne waliopendekezwa kuhudumu katika wa Bodi ya Utumishi wa Umma katika Bunge la Kaunti ya Murang’a.
Bunge la Kaunti ya Murang’a limepewa muda wa siku 21 kuanzia Juni 17 kubaini hatima ya watu hao watano.
Endapo Dkt Macharia ataidhinishwa kwa wadhifa huo, Dkt Macharia atasimamia huduma za watumishi wa umma katika bunge la Murang’a kama vile, uajiri, utathmini wa utendakazi na masuala ya nidhamu.
Ni majukumu yaya haya ambapo alitekeleza katika TSC kwa miaka 10.
TSC mnamo Juni 1, 2025 ilimteua Eveleen Mitei kuwa kaimu afisa mkuu mtendaji kuchukua mahala pa Dkt Macharia.
Bi Mitei amekuwa akihudumu kama Naibu Mkuu wa Idara ya Huduma za Wafanyakazi.