Habari

Sheria ya Urithi inayobagua waume waliofiwa yaharamishwa

Na SAMSON KIPLAGAT June 21st, 2025 Kusoma ni dakika: 2

MAHAKAMA Kuu imeamua kwamba sehemu fulani ya Sheria ya Urithi inakiuka haki kwa kuhitaji wanaume waliofiwa na wake wao kuthibitisha kuwa walikuwa wakiwategemea wake hao ili waruhusiwe kurithi mali ya marehemu.
Jaji Lawrence Mugambi alisema sehemu ya 29 (c) ya sheria hiyo inawabagua wanaume kwa sababu sharti hilo, la kutakiwa kuthibitisha ikiwa walikuwa wakiwategemea wake wao, halijawekewa wajane.
Jaji huyo alisema kuwa sehemu hiyo, ya sheria, inakiuka katiba kwani inaleta ubaguzi kati ya wanaume na wanawake.
“Nimebaini kuwa neno “mtegemeaji” limepewa maana ya kubagua Sehemu ya 29 (c ) ya Sheria ya Urithi inapomtaka mume wa mwanamke aliyekuwa kuthibitisha kuwa alimtegemea ilhali sharti kama hilo halihitajiki chini ya Sehemu ya 29 (a ) ya sheria hiyo kwa mke wa mwanamume aliyekufa. Kwa hivyo, sehemu ya 29 (c) inakiuka katiba,” akasema Jaji Mugambi.
Jaji Mugambi aliongeza kuwa uamuzi huo haufai kueleweka kumaanisha kuwa mahakama imeharamisha “hitaji la kuthitibisha kuwa mtu fulani alikuwa akimtegemea mwenzake katika ndoa.”
“Lakini endapo patahitajika kwamba mmoja wa wanandoa athibitishe kuwa alimtegemea mwenzake, hitaji hilo litakuwa halali. Hata hivyo, mahakama hii inaharamisha hali ambapo mmoja wa wanandoa anabaguliwa katika suala la urithi wa mali baada ya mwenzake kufa,” akafafanua Jaji Mugambi.
Jaji huyo alisisitiza kuwa sehemu ya 29 (c) ya sheria ya Urithi inambagua mume ambaye mkewe alikufa bila kuacha wosia.
Katika kesi hiyo afisa wa mahakama aliyetambuliwa kama DKM alilalamika kuwa sehemu hiyo ya sheria haimtendei haki kama mume kwa sababu inamhitaji kuthibitisha kuwa alimtegemea marehemu mkewe kabla ya kifo chake ili aruhusiwe kufaidi kutokana na mali ya mwendazake.
Afisa huyo alisema kuwa wake ambao waume wao walikufa hawajawekewa sharti kama hilo.
Bw DKM alisema kuwa Sheria ya Urithi iliundwa mnamo 1981 na inapasa kuoanishwa na Katiba ya sasa.
Kupitia wakili wake Shadrack Wambui, alisema kuwa sehemu ya 29 ni muhimu zaidi katika Sheria ya Urithi kwani inatumika kuamua yule atakayefaidi au kurithi mali ya mtu aliyekufa.
Jaji Mugambi alisema kuwa sehemu hiyo katika sheria hiyo inabagua kati ya mwanandoa ambaye ni mume.
Hii ni licha ya kwamba sehemu ya 29 (a) ya sheria hiyo inasema kuwa wategemeaji sio “mke au wake, mke au wake wa zamani, na watoto wa mwendazake.
Inasisitiza kuwa watu hawa watafaidi bila kujali kwamba walitunzwa na marehemu kabla ya kifo chake au la.