Kimataifa

Vita Sudan vyageuka wapiganaji wa RSF wakianza kujiunga na jeshi la serikali

June 24th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KHARTOUM, Sudan:

HATUA ya baadhi ya wapiganaji wa RSF kuhama na kujiunga na wanajeshi wa Sudan imezua ghadhabu na ukosefu wa uthabiti nchini humo.

Baadhi ya raia wamekasirishwa na kuhama huko wakisema kuwa makamanda wa RSF ambao wamefanya hivyo sasa watakwepa uwajibikaji wa kisheria ilhali wametendea raia madhila na hata kusababisha mauaji.

Mwezi uliopita, Ali Rizkallah, kamanda wa RSF alikaribishwa jijini Khartoum na kupewa sare pamoja na cheo katika ngazi ya juu ya jeshi la Sudan.

Ali alikuwa amepigania RSF kwa miaka mitatu, akiwa kati ya makamanda ambao wameshutumiwa kwa mauaji, ubakaji na maovu mengine jijini Darfur.

“Siwezi kuwasamehe hawa wapiganaji wa RSF hata wakiomba msamaha kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Siwezi kuwasamehe kutokana na kile ambacho nilikiona kwa macho yangu,” akasema Halima Ismail, mwanamke kutoka mashariki mwa Darfur.

Alirejelea tukio ambalo wapiganaji walioongozwa na Ali walipiga risasi hewani wakati wa uvamizi kwenye kijiji ambacho walikuwa wamejikinga mnamo 2024.

Vita Sudan vinaaminika kuchangia katika vifo vya maelfu ya watu, kusababisha wengine mamilioni kuhama na kuchangia kusambaa kwa magonjwa na njaa.

RSF walikosana na wanajeshi wa serikali na wakaanza kupigana mnamo Aprili 2023.

Baadhi ya visa katili zaidi vya ukiukaji wa haki za binadamu vimetokea Darfur, ngome ya RSF ambako Ali maarufu kama Al-Savannah, alikuwa kamanda wa Darfur.

RSF imeshutumiwa kwa uvunjaji wa haki za binadamu katika jiji la Al-Fashir tangu Oktoba.

Mnamo Aprili, kamanda mwingine wa RSF Kaskazini mwa Darfur Al-Nour Guba pia alijiunga na wanajeshi wa serikali.

Guba alikanusha kuwa alihama ili kukwepa haki na kusema kuwa kamanda yeyote wa RSF ambaye alishiriki dhuluma anafaa kuwajibikia vitendo vyake.

“Iwapo raia yeyote wa Sudan ana malalamishi na ushahidi dhidi yetu, basi tuko tayari kujitetea hasa kuhusu madai ya kuvunja haki za binadamu,” akasema.

Ali mwenyewe alisema yuko tayari kujisalimisha iwapo kuna ushahidi alishiriki mauaji na dhuluma nyingine dhidi ya raia.

Jeshi la Sudan na RSF, wote wamekanusha kuwa walishiriki mauaji ya raia Darfur.

Mkazi wa kijiji cha Tawila, Darfur, Ismail alisema kuwa alilazimika kuhama kila mara RSF ilipovamia vijiji karibu na Al-Fashir.

Alisema aliwaona wanawake wakibakwa mbele yake na akatandikwa na wapiganaji hao hao wa RSF.

“Unaweza kuona alama za majeraha kwenye mkono wangu, mpaka chini kwa miguu yangu,” akasema.

Katika mojwapo ya matukio chini ya amri ya Ali, wapiganaji walifyatua risasi hewani na kumlazimu Ismail na wanawe walale chini.