Habari

Wito viongozi waache siasa za ukabila

Na WINNIE ONYANDO June 22nd, 2025 Kusoma ni dakika: 1

RAIS wa Bunge la Mwananchi ametoa wito kwa viongozi wa upinzani kuepuka siasa za ukabila.

Akizungumza Jumamosi Juni 21, 2025 katika bustani wa Jivanjee Nairobi, Bw Awino alisema kuwa ni jambo la kushangaza kuwa upande wa upinzani ukiongozwa na aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua unajiuhusisha na siasa za kuleta mgawanyiko badala ya kuwaunganisha Wakenya.

“Siasa za ukabila ni tishio kwa umoja wa nchi,” akasema Bw Awino.

Kando na hayo, alisema kuwa siasa za Kenya zikichukua mkondo kama huo, basi ustawi wa nchi utakwama kwani watu wakija pamoja bila kujali kabila, wanaweza kutimiza makubwa.

“Tunaposhinda tu tukisema kuwa Wakikuyu ndio wanafaa au Waluo ndio wanafaa kuwa serikalini, basi hii ni kama kuleta vita na vurugu nchini.”

Alimtaka Bw Gachagua na viongozi wengine wa upinzani kuwajibisha serikali badala ya kujihusisha na siasa za ukabila.

“Ukienda kujipigia debe mahali, unachofaa kufanya ni kuwashawishi wapiga kura na kuuza ajenda zako sio kuuza sera za kikabila,” akaongeza Bw Awino.

Haya yanajiri siku chache tu baada ya Bw Awino kuzindua vuguvugu la Kenya Moja Coalition linalolenga kuwaunganisha Wakenya.