Habari za Kitaifa

Familia ya polisi aliyetoweka Haiti yaishtaki serikali

Na NYABOGA KIAGE June 23rd, 2025 Kusoma ni dakika: 2

FAMILIA ya afisa wa polisi wa Kenya aliyetoweka mnamo Machi 25, 2025 baada ya makabiliano ya risasi kati ya walinda usalama wa Kenya na genge moja nchini Haiti imeishtaki serikali.

Inataka iambiwe kilichomtendekea mpendwa wao Benedict Kabiru na kwa nini maafisa asasi husika hawajatoa maelezo kuhusu hatima yake.

Mwanasheria Mkuu Dorcas Oduor, Waziri wa Usalama Kipchumba Murkomen, Inspekta Jenerali wa Polisi Douglas Kanja na Mkuu wa Mawaziri Musalia Mudavadi wameorodheshwa kama washtakiwa katika kesi hiyo.

Familia hiyo inasema haijapata ufafanuzi kuhusu kile kilichomtendekea Bw Kabiru.

Sasa imechanganyikiwa baada ya Baraza la Kuu la Mpito nchini Haiti kudai Kabiru aliuawa ilhali serikali ya Kenya ikishikilia kuwa afisa huyo alitoweka tangu siku ambayo kikosi cha Kenya kilikabiliana na wanachama wa genge la wahalifu.

“Inspekta Jenerali wa Polisi na Waziri wa Usalama hawajafafanua kauli hizi za kukanganya na wameendelea kunyima familia ya Benedict Kabiru Kuria taarifa kamili kuhusu hatima ya mpendwa wao,” kesi hiyo iliwasilishwa na kampuni ya Mawakili ya Gathenji ilisema.

Inaeleza kuwa walalamishi ambao ni Jacinta Wanjiku Kabiru (mamake afisa huyo), Daniel Kabiru Ndung’u (mjomba) na Philip Kamau Kuria (kakake afisa huyo) walimuuliza Mkurugenzi wa Operesheni katika Huduma ya Kitaifa ya Polisi (NPS) Ranson Lolmodoni afafanue ikiwa Kabiru yu hai au la.

Lakini Bw Lolmodoni alipuuzilia mbali ripoti kwamba alikufa akisema hizo ni habari za uongo zinazoendelezwa katika mitandao ya kijamii.

“Majaribio ya jamaa kupata ukweli kuhusu hali ya Benedict Kabiru Kuria baada ya hapo hayajafaulu kwani washtakiwa walionyesha mapuuza na hawakutoa majibu ya wazi,” inaeleza hati ya kesi hiyo.

Kulingana na kesi hiyo, sheria kadhaa zimekiukwa sawa na Katiba ya Kenya kwa serikali kufeli kuelezea aliko Kabiru.

Kesi hiyo inataja Kipengele cha 12 cha Mkataba Ulimwengu kuhusu Haki za Kibinadamu (UDHR) unaosema kuwa familia inayo haki ya kupata maelezo yoyote kuhusu mpendwa wao.

Kwa hivyo, kulingana na walalamishi katika kesi hiyo washtakiwa hawajakuwa wakitoa maelezo kuhusu aliko Kabiru au juhudi ambazo zinaendeshwa kusaka na hatua ambayo imepigwa kufikia sasa kumpata au kumwokoa.

“Isitoshe, kuna maelezo ya kukanganya kutoka Haiti kuhusu afisa huyo wa polisi yanayodai kuwa amekufa. Na kwa upande mwingine washtakiwa wanashikilia kuwa afisa huyo wa polisi angali hai na wanamsaka,” stakabadhi za kesi hiyo zinaeleza.