Walimu wakataa nyongeza ya Sh8.4 bilioni, wasema nyongeza nzima inamezwa na ushuru
WALIMU nchini wamekataa nyongeza ya mishahara ya awamu ya pili ya Mkataba wa Pamoja wa Ajira (CBA) wa miaka ya 2025–2029, wakisema ni ndogo mno wala haiendani na gharama ya maisha inayozidi kupanda.
Malalamishi hayo yameibuka baada ya Tume ya Kuajiri Walimu (TSC) kutoa barua inaoyoelekeza utekelezaji wa awamu ya pili ya mkataba huo kuanzia Julai 1, 2026.
Walimu wengi waligundua kuwa nyongeza yao halisi ni kati ya Sh693 na Sh2,055 pekee kulingana na cheo na kiwango cha mshahara.
Ingawa serikali ilitenga Sh8.4 bilioni kutekeleza awamu hiyo, walimu wanasema kiasi kinachoingia katika akaunti zao baada ya makato ya kisheria hakina tofauti kubwa na mshahara wa awali.
“Mwalimu wa daraja ya C3 alitarajiwa kuongezewa Sh2,055, lakini hiyo ni kabla ya makato ya PAYE, SHA, Ushuru wa Nyumba na NSSF. Kinachobaki ni kidogo sana na hakiwezi hata kusaidia kulipa mkopo wa SACCO,” alisema mwalimu mmoja wa Nairobi.
Mkataba huo wa miaka minne una thamani ya Sh33.75 bilioni, ukihusisha nyongeza ya mishahara na masuala ya ustawi wa walimu.
Hata hivyo, walimu wengi sasa wanasema matarajio yaliyotolewa na vyama vyao hayalingani na hali halisi.
Katibu wa KUPPET tawi la Vihiga, Sabala Inyeni, alisema nyongeza hiyo haijazingatia mfumuko wa bei wala kupanda kwa gharama za usafiri.
“Marupurupu ya usafiri hayajabadilishwa kwa zaidi ya miaka 15 ilhali bei ya mafuta imeendelea kupanda. Ongezeko hili haliendani na hali halisi ya maisha,” alisema.
Walimu wanaofanya kazi katika maeneo magumu na kame pia wameeleza kutoridhishwa kwao baada ya marupurupu ya mazingira magumu kukosa kuongezwa.
Katibu wa chama cha walimu wanaohudumu katika maeneo hayo Ndung’u Wangenye, alisema baadhi ya walimu wameongezewa chini ya Sh500 huku wakifanya kazi katika mazingira magumu.
“Walimu wa maeneo kame wanahisi wamesalitiwa. Marupurupu ya mazingira magumu ndiyo yanayowatia moyo kuendelea kufanya kazi huko, lakini hayajaguswa kabisa,” alisema.
Naibu Katibu Mkuu wa KUPPET Moses Nthurima, alisema walimu wengi hawajaridhishwa na matokeo ya mazungumzo ya CBA.
“Serikali imechukua fedha nyingi kupitia makato ya SHA, ushuru wa nyumba, NSSF na kodi kuliko ilivyorejesha kupitia nyongeza ya mishahara. Ndiyo maana walimu hawaoni faida ya ongezeko hili,” alisema.