Makala

Mzee aliyeondoka nyumbani 1965 na kwenda Uganda arejea mikono mitupu

Na SHABAN MAKOKHA  June 23rd, 2025 Kusoma ni dakika: 2

WAKAZI wa kijiji cha Eshisari, Mumias Mashariki Kaunti ya Kakamega walipatwa na mshangao baada ya mzee mwenye umri wa miaka 99 aliyeondoka nyumbani miaka 60 iliyopita kurejea.

Boniface Muhandia aliondoka nyumbani kwao mnamo 1965, akiwa na umri wa miaka 39 na kuelekea Uganda.

Sasa akiwa mzee, amerejea nyumbani baada ya watu wa familia yake kumsaka kwa miaka kadhaa na kudhani huenda alifariki.

Muhandia alisema amekuwa akiishi Uganda ambako alipata ajira na kuishi maisha mazuri lakini akarejea nyumbani bila mali yoyote.

Baba huyo wa watoto sita alirejea mwishoni mwa wiki na mkongojo na sanduku dogo, mali ya kipekee aliyopata akiishi Uganda kwa zaidi ya miongo sita.

Ni watu wachache wa familia yake waliweza kumkumbuka.

Mkewe na watoto wake wawili wa kiume waliaga dunia na wakazikwa na wanawe waliosalia hawawezi kumtambua baba yao huyo.

Baada ya kuhitimu kama mwashi, hakubahatika kupata kazi nchini Kenya na ndipo akahamia Uganda kusaka ajira ya mshahara mzuri wa kusaidia kutunza mkewe na watoto.

Mzee Boniface Muhandia, 99, aliyeondoka nyumbani kwenda Uganda miaka 60 iliyopita, arejea nyumbani kwa mkongojo akiwa hana chochote. Picha|Shaban Makokha

Mzee Muhandia aliyezaliwa mwaka wa 1926, alisema kwanza alitua katika mji wa Busoga kabla ya kuhamia jiji la Kampala ambako aliishi hadi juzi alipoamua kurejea nyumbani.

“Nilifanya kazi kwa muda mrefu zaidi jijini Kampala na watu walinipenda kwa bidii na kazi yangu nzuri. Hii ndiyo maana niliweza kuisha Uganda kwa muda huo wote,” akaeleza.

“Nimerejea nyumbani kutafuta watu wa familia yangu lakini nashangaa kuwa wengi wao walikufa na kuzikwa nikiwa Uganda. Nilijua kwamba ningerudi kujumuika nao lakini sikujua kwamba ningewakosa baadhi ya watoto wangu na mke wangu,” akasema.

Ingawa mkewe, Kelemendia Adhiambo, alimfuata Uganda mwishoni mwa 1970, alirejea nyumbani kuwatunza watoto baada ya kukaa kwa muda mfupi katika nchi hiyo jirani.

Akiwa Uganda, alijaliwa watoto wawili, wa kiume na kike, na akarejea nyumbani na watoto hao.

Watoto wawili wa kiume wa Mzee Muhandia walikufa mwishoni mwa miaka ya 1990s, ilhali mkewe alikufa miaka miwili iliyopita na hakuhudhuria mazishi yake.

“Ingawa nilikuwa nikiwasiliana na familia yangu kwa barua nilizozituma kupitia shirika la posta nchini, baadaye nilipoteza mawasiliano nao na ndiyo maana sikupata habari za vifo vya baadhi yao,” aliongeza.

Mzee Muhandia ambaye alionekana kuchanganyikiwa, hakumbuki siku ya mwisho ambayo aliwasiliana na mkewe pamoja na watoto.

Sasa kitinda mimba wake, Protus Makokha, anapanga kumjengea nyumba.