Aliacha bodaboda kuzamia ufugaji wa mbuzi wa nyama
KILA saa sita mchana kijiji cha Nyanguru, eneobunge la Nyaribari Chache, Kaunti ya Kisii, Mike Mose, 35, husikika akiita mbuzi wake kwa sauti kubwa.
Mikononi mwake amebeba majani ya kuwalisha. Mbuzi 87 hukimbia kwa fujo wakimjua ndiye anayewalisha.
Miaka saba iliyopita, taswira ilikuwa tofauti. Mose alikuwa mwenyekiti wa wanabodaboda mjini Kisii.
Kwa miaka mitano, alisimamia vijana zaidi ya 1,000 na kujua barabara zote za mji huo.
Alistaafu bodaboda mwaka 2021 baada ya janga la corona na kupanda kwa mafuta kumaliza kipato.
“Nilikuwa nikifanya kazi ya bodaboda kutoka saa kumi na mbili asubuhi hadi saa kumi jioni. Lita moja ya mafuta ilikuwa 140. Ukitoa chama, ukitoa za polisi, ungebaki na 400,” anakumbuka.
Alipouza pikipiki yake alibaki na Sh50,000, watoto wawili shuleni, na miezi minne bila kazi.
Aliporejea kijijini, afisa mmoja wa mifugo ambaye ni rafikiye, alimpa ushauri, “Wewe unajua kuongoza watu. Ongoza mbuzi sasa. Wanakua haraka, soko lipo hasa wakati wa sherehe kama zile za Idd, Ramadhan, Pasaka na Krismasi.”
Bila kusita, alianza na mbuzi watatu wa kike aina ya Galla na dume mmoja aina ya Saanen kwa Sh18,000.
Kwa wakati huu, ana mbuzi 87 wa nyama na anapanga kuwauza wakati wa shamrashamra za mwezi Desemba ikiwemo Krismasi.
Mose huwaachilia mbuzi wake kusaka malisho katika nusu ekari ya shamba lake.
Mbuzi hao hulishwa kwa nyasi za napier, mchicha wa mbuzi, na mabaki ya viazi kutoka kwa wauzaji wa vibanzi au maarufu chipsi.
Gharama ya mbuzi hawa kwa mwezi kulingana na Mose ni Sh20,000 tu, kwa ajili ya dawa, chumvi, na mshahara wa kijana mmoja anayesaidia kusafisha banda.
“Kwa bodaboda, siku mbaya unarudi na Sh200. Mbuzi hawali mafuta,” anacheka.
Mbuzi wa kike huzaa mara mbili kwa mwaka, na mara nyingine wao huzaa pacha. Juhudi zake zimefanikiwa kwani yeye pia huendelea kununua mbuzi wengine wa kufuga.
Ana mbuzi dume 27 ambao anataka watimize uzani wa sokoni kabla ya kuwauza ndani ya miezi mitano ijayo.
Ili kutimiza hilo, ameanza kuwalisha unga wa mahindi na dagaa ili wafikie kilo 30 kabla ya sikukuu, kwa sababu wateja hawataki mbuzi wadogo.
Uzoefu wake wa bodaboda ndio soko lake kubwa.
“Nilikuwa najua wachinjaji wote mjini Kisii kwa sababu walikuwa wanapanda pikipiki yangu. Leo nina nambari zao za simu. Nikituma picha ya mbuzi WhatsApp, mteja anasema ‘Leta watano kesho,'” anaeleza.
Desemba mwaka jana aliuza mbuzi 52 kwa siku 10 pekee.
Mteja mmoja alitoka Nairobi akachukua 20, hoteli moja Kisii ikachukua 15, na jumla yake ilikuwa Sh980,000.
Baada ya kutoa gharama, faida ilikuwa Sh620,000. Pesa hizo alizitumia kulipia wanawe karo shuleni, akanunua mabati ya nyumba mpya, na akabakisha Sh150,000 kama mtaji.
Mwaka huu analenga mbuzi 60 kwa Sh1.2 milioni, na anatarajia faida ya Sh750,000.
Uongozi wa bodaboda ulimfundisha nidhamu anayoitumia sasa. Kanuni yake ya kwanza ni kusubiri bei ipande.
Agosti na Septemba mbuzi ni Sh15,000, lakini Novemba hadi Desemba bei inapanda kwa asilimia 30 hadi zaidi ya Sh20,000.
Pili ni uzito. Anapima kila Jumamosi kuhakikisha dume wanaofikisha kilo 30 na kuendelea.
Tatu ni kuweka oda mapema. Kama alivyopanga safari za bodaboda, sasa anapanga mauzo.
Kutoka Oktoba anashika namba za wachinjaji na mahoteli ili Desemba mbuzi wake wawe tayari wamepata soko. Yeye hutumia makundi ya WhatsApp kuweka picha za mbuzi anaowauza.
Hata hivyo, safari yake sawa na nyingine nyingi, hazijakuwa bila changamoto.
Mnamo 2024, mbuzi wake 14 walikufa baada ya kuathiriwa na ugonjwa. Tukio hilo lilimtia wasiwasi na kumkumbusha wakati ambapo pikipiki yake pia ilipata hitilafu.
“Lakini nilijifunza. Sasa napiga chanjo kila baada ya miezi 3. Huwa nalipa Sh50 kwa kila mbuzi,” anasema.
Wezi pia walimjaribu, lakini banda lake la mabati na taa ya sola pamoja na mbwa wake wakali waliwafukuza.
Mose bado ni kiongozi, lakini sasa kwa njia nyingine. Kila siku huwalisha mbuzi mara mbili, asubuhi na mchana. Atakapowauza Desemba, ataongeza wengine Januari ili kuendeleza biashara yake.
“Siwezi kusema mimi ni tajiri. Lakini kutoka bodaboda hadi mbuzi, Mungu ameniinua,” anasema.
Ushauri wake kwa vijana wa bodaboda ni mfupi.
“Wapange mustakabali kwa sababu bodaboda ni kazi sio maisha, na ekari nusu na mbuzi watano ni bora kuliko kukosa kazi ukiwa na umri wa miaka 40. Watumie mtandao wao kwa sababu wateja wao ni wale wanawabeba kila siku na waanze chini. Wasiruke kununua mbuzi 50 mara moja,” anashauri Mose.
Anamaliza akimbembeleza mbuzi dume mkubwa aliyefunga kamba nyekundu na kumuita ‘Bonus’ kwa sababu atamlipia shule ya mtoto wake mkubwa.