Habari

Maandamano ya GenZ yaanza kwa amani Mombasa

Na WINNIE ONYANDO June 25th, 2025 Kusoma ni dakika: 1

MAANDAMANO ya Juni 25, 2025 ya kuadhimisha mwaka mmoja tangu wanarika wa GenZ kuuawa kikatili na polisi yalianza kwa amani katika baadhi ya kaunti.

Katika Kaunti ya Mombasa, waandamanaji hao waliofika kwa wingi walionekana wakibeba mabango yaliyoandikwa jumbe za kudai haki huku wakitembea kwa umoja bila vurugu.

Baadhi ya picha zinaonyesha waandamanaji wakiwa katika shughuli zao bila kuvurugana na maafisa wa polisi waliokuwa wakiimarisha usalama.

Kwa upande mwingine, maandamano hayo pia yalianza kwa amani katikati mwa jiji la Nairobi huku nyimbo za kudai haki kwa waathiriwa wa ukatili wa polisi zikitawala.

Hata hivyo, kadri watu walivyoongezeka katikati mwa jiji la Nairobi ndivyo maafisa wa usalama walivyoongezwa ili kukabiliana na waandamanaji hao.

Katika Kuanti ya Kisumu, maandamano hayo pia yalianza kwa amani huku waandamanaji wakidai haki kwa wale waliouawa mikononi mwa polisi.

Maandamano hayo pia yalishika kasi katika kaunti za Embu, Machakos, Uasin Gishu, Makueni, Nakuru, Nyeri, Kajiado na Kisii.