Kaunti za North Rift zalemewa na madeni – Ripoti
MAGAVANA kutoka kanda ya kaskazini mwa Bonde la Ufa wanakabiliwa na shinikizo la kulipa madeni ya mamilioni ya pesa huku ripoti za ukaguzi wa fedha zikionyesha jinsi fedha zilizotengewa maendeleo hazijatumika ipasavyo.
Serikali za kaunti katika kanda hiyo zimeshutumiwa kwa kuchelewesha malipo kwa wanakandarasi na wawasilishaji wa bidhaa.
Hata hivyo, ufisadi katika tawala zilizopita kwenye gatuzi hizo zimechangia kaunti kushindwa kujimudu kifedha.
Katika Kaunti ya Turkana utawala wa Gavana Jeremiah Lomorukai umetenga Sh1.02 bilioni katika mwaka wa fedha wa 2026-2027 kulipa madeni ya wanakandarasi na wawasilishaji bidhaa.
“Tunafahamu kuna kazi ambazo zimekamilika lakini bado hazijalipwa na hatuna jingine ila kulipa,” akasema Waziri wa Fedha wa Kaunti ya Turkana Roseline Aite wakati akiwasilisha makadirio ya bajeti ya Sh17.9 bilioni.
Katika Kaunti ya Trans Nzoia serikali ya gatuzi inalenga kukusanya Sh1 bilioni kama mapato katika mwaka wa kifedha wa 2026-27 ili kuboresha huduma.
Gavana George Natembeya amesema ukusanyaji mdogo wa mapato umechangiwa na mianya katika mfumo.
Kwa mujibu wa Mamlaka ya Ugavi wa Mapato (CRA), Trans Nzoia ina uwezo wa kujikusanyia hadi Sh1.8 bilioni.
Kaunti ya Nandi imewasilisha bajeti ya Sh3.89 bilioni ambayo msingi wake ni uwekezaji katika sekta za afya, elimu, ujenzi wa barabara na miradi ya maji.
Serikali ya Kaunti ya Uasin Gishu nayo imewasilisha pendekezo la bajeti ya Sh12.99 bilioni kwa mwaka wa fedha wa 2026-2027 bila kuongeza ushuru na ada nyingine.
“Tumeboresha mfumo wa ukusanyaji mapato ili kutimiza lengo letu la kuzoa Sh1 bilioni,” akasema Bw Natembeya.
“Ripoti ya CRA inaonyesha tunaweza kukusanya hadi Sh900 milioni kama mapato ya ndani. Lazima tuzibe pengo kati ya kiwango tunachokusanya sasa na uwezo tulionao,” akaongeza bosi huyo wa kaunti.