Makala

‘Bwana Spika Sir’ ashtakiwa kwa uvamizi wa Bunge 2024 na uharibifu wa mali ya Sh41m

Na RICHARD MUNGUTI June 30th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MWANAHARAKTI Ezekiel Kyama Nzyoki aliyefaulu kuingia katika jengo la Bunge huku akimuiga Spika wa Bunge la Kitaifa Juni 25, 2024 akisema “Bwana Spika Sir”, ameshtakiwa hatimaye baada ya kukwepa mtego wa polisi miaka miwili kwa kuharibu mali ya bunge ya Sh41 milioni.

Mwanaharakati huyo shupavu alijirekodi pamoja na wenzake wakila wali na maankuli mengine katika bunge la kitaifa.

Wanaharakati wa Gen Z waliwazidia nguvu maafisa wa usalama na kuingia katika jengo la Bunge wakati wa maandamano hayo ya kupinga Mswada wa Fedha 2024.

Tukio hilo liliwatia wabunge woga na hofu kuu hata wakatorokea shimo linalounganisha jengo la Bunge Towers na Bunge lenyewe.

Bw Nzyoki ambaye ni mwanafunzi wa chuo kikuu, mwenye umri wa miaka 22 alishtakiwa katika mahakama ya Milimani mwendo wa saa sita unusu mchana Juni 29, 2026.

Mwanaharakati Ezekiel Kyama Nzyoki aliyeshtakiwa Juni 29, 2026 kwa kuvamia Bunge akiwa na Gen Z wengine Juni 25, 2024.
Picha|Richard Munguti

Mwanaharakati huyo alipata umaarufu mwingi baada ya video aliyojichukua akiwa ndani ya Bunge akisema “Bwana Spika Sir” kusambazwa na vyombo vya habari na mitandao ya kijamii mnamo Juni 25, 2024.

Nzyoki alikabiliwa na mashtaka mawili ya kuingia katika jengo la Bunge bila idhini na kukiuka sheria nambari 31 (1)(a) na 32 (2) zinazolinda jengo hilo linalokuwa chini ya ulinzi mkali.

Shtaka la pili lilikuwa la kuharibu mali katika majengo hayo zikiwamo sahani, vikombe, kamera za CCTV na mitambo ya mawasiliano yote ya thamani ya Sh41,248,570.

Mawakili Gordon Ogada na Babu Owino waliomba mahakama imwachilie Nzyoki kwa dhamana isiyo ya kiwango cha juu.

Ogada alimweleza hakimu kwamba polisi walimtia nguvuni Nzyoki aliposhtakiwa mbele hakimu mkuu Teresia Nyagena wakati wanaharakati zaidi ya 200 waliposhtakiwa.

Mahakama ilielezwa Nzyoki na wenzake walilipiwa dhamana na aliyekuwa Gavana wa Nairobi Mike Sonko.

Waandamanaji hao wa wiki jana waliokuwa wanafanya kumbukumbu ya watu zaidi ya 60 waliouawa na polisi kwa kupinga Mswada wa Fedha wa 2024-2025 walitiwa mbaroni na polisi.

Miongoni mwao alikuwa Nzyoki.

Mshtakiwa huyo alisubiriwa na polisi na kutiwsa nguvuni alipokuwa anaenda nyumbani.

Alizuiliwa na hatimaye akifishwa kortini Juni 29, 2026.

Wakili Babu Owino (katikati) azugumza na wanahabari baada ya kumtetea mwanaharakati Ezekiel Kyama Nzyoki aliyedaiwa aliingia bungeni Juni 25, 2024. Picha|Richard Munguti

Alikana mashtaka dhidi yake na kueleza mahakama kwamba “peke yake hawezi kuharibu mali ya Sh41.2 milioni ndani ya jengo la bunge.”

Mahakama iliombwa isizingatie habari za upande wa mashtaka kwa vile mshtakiwa hawezi kutoroka na hakuna ushahidi wowote uliowasilishwa kuthibitisha atawavuruga mashahidi.

Upande wa mashtaka haukupinga Nzyoki kuachiliwa kwa dhamana.

Hakimu mwandamizi Carolyne Mugo alimwachilia mshtakiwa kwa dhamana ya Sh100,000 na kuamuru upande wa mashtaka umkabidhi mshtakiwa nakala za mashtaka.

Kesi itatajwa baada ya wiki mbili.

Nzyoki alidhaminiwa na baba yake na kutoka kizuizini.