Habari

Wavamizi warejea kutishia tena manusura wa kijiji kilichochomwa 2022

Na SAMMY LUTTA June 26th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

WIKI tatu pekee baada ya serikali ya Kaunti ya Turkana kuwahamisha manusura wa shambulio katika kijiji cha Napeitom lililotekelezwa na wavamizi Julai 2022 katika eneo la Suguta na kuacha wengi bila makao, wahalifu hao wamerejea na kuanza tena kutisha wakazi.

Mnamo Jumatatu, wavamizi waliwaua watu wawili na kuwajeruhi wengine wawili, hali iliyofufua kumbukumbu za shambulio la mwaka 2022.

Familia 101 za watu wapatao 800 ambao walifurushwa wakati wa shambulio hilo bado hawajarudi kijijini.

Wakazi wa kijiji hicho walikimbia baada ya shambulio hilo ambalo watu saba waliuawa na kuhamia Lokori, takribani kilomita 35 kutoka kijiji hicho.

Walirudi mapema mwezi huu baada ya serikali ya kaunti kujenga nyumba 30 za kudumu na kuweka ua, lango na mnara wa ulinzi ili kulinda kijiji hicho kipya.

Serikali ya kaunti pia ilikarabati zahanati, kisima cha maji na shule ya chekechea katika kijiji hicho kipya.

Kulingana na Naibu Kamishna wa Kaunti Ndogo ya Suguta, Franklin Ongori, wavamizi walilenga watu watatu waliokuwa wakielekea Lokori kwa pikipiki, ambapo wawili waliuawa papo hapo na wa tatu kujeruhiwa kwenye nyonga ya kushoto.

Waliouawa walitambuliwa kama Salin Asiyer na Ekaran Inok.

Walioumia walipelekwa haraka katika Hospitali ya Kaunti Ndogo ya Lokori kabla ya kuhamishiwa katika Hospitali ya Rufaa ya Kaunti mjini Lodwar.

Mapema siku hiyo, wahalifu hao walishambulia wachungaji waliokuwa wameondoka kijijini kuelekea maeneo ya malisho, ambapo mmoja alijeruhiwa mkononi.

“Maafisa wa usalama kijijini ambao walikuwa macho waliwazima wavamizi hao,” alisema Bw Ongori.

Naibu Kamishna huyo alisema mtu mmoja aliokolewa na wanajeshi wa KDF waliokuwa wakishika doria kwa usaidizi wa droni.

Alisema doria zimeimarishwa kwa msaada wa wanajeshi wa KDF na kuwataka wakazi kuwa na imani na maafisa wa usalama kuwalinda.

Mmoja wa manusura, Loris Lopur, ambaye alinusurika na majeraha, alisema kuwa kama si kwa droni ya KDF, angeuawa pia.

Alielezea jinsi alivyojificha kwenye kichaka kando ya barabara ya Napeitom-Lokori na jinsi droni hiyo ilivyomwelekeza kwenye gari la kivita la KDF.

“Wavamizi waliwapiga risasi na kuwaua watu wawili waliokuwa kwenye pikipiki nyuma yangu. Walinyang’anywa mali pia. Nilipokuwa nikikimbia bila viatu, niliona droni ya KDF iliyowatisha wavamizi waliokuwa wakitaka kuniua. Niliamua kufuata mwelekeo wa droni hadi nikafika kwa gari la wanajeshi. Walinipa maji na kunipeleka hospitalini,” alisema Bw Lopurn akiwa katika Hospitali ya Rufaa ya Kaunti ya Lodwar.

Aliongeza kuwa alipelekwa kwanza katika Hospitali ya Kaunti Ndogo ya Lokori kabla ya kuhamishiwa Lodwar.