WALIOBOBEA: Andrew Omanga alitikisa sana siasa za eneo la Gusii miaka ya themanini
ANDREW John Omanga alijijengea jina kama mmoja wa wanasiasa waliokuwa na ushawishi mkubwa katika eneo la Gusii licha ya kuepuka umaarufu wa kisiasa uliokuwa na viongozi wenzake.
Alikuwa mbunge wa Nyaribari, waziri katika serikali za marais Jomo Kenyatta na Daniel arap Moi, na mmoja wa watumishi wa umma waliobobea kabla ya kuingia rasmi katika siasa.
Safari yake ya kisiasa ilianza mwaka 1979 alipochaguliwa kuwa Mbunge wa eneo kubwa la Nyaribari baada ya kumshinda Lawrence Sagini katika uchaguzi mkuu.
Ushindi huo ulimfungulia mlango kuingia katika Baraza la Mawaziri la kwanza la Rais Daniel arap Moi, aliyekuwa amechukua mamlaka baada ya kifo cha Mzee Jomo Kenyatta mwaka 1978.
Omanga aliingia serikalini kwa ushawishi wa aliyekuwa Katibu Mkuu wa Utumishi wa Umma, Simeon Nyachae, ambaye wakati huo alikuwa mmoja wa maafisa wenye nguvu zaidi serikalini.
Katika baraza hilo jipya pia walikuwamo Nicholas Biwott, Moses Mudavadi, Joseph Kamotho, Charles Rubia, John Okwanyo, G.G. Kariuki, Arthur Magugu, Jonathan Ng’eno na Kabeere M’Mbijjewe.
Rais Moi alisema serikali yake mpya ingeweka mkazo katika kujenga taifa na kuboresha utendaji wa serikali.
Omanga aliteuliwa kuwa Waziri wa Mazingira na Maliasili kabla ya baadaye kuhamishiwa Wizara ya Viwanda.
Aliyekuwa Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Jomo Kenyatta cha Kilimo na Teknolojia, Profesa Ratemo Michieka, alikumbuka Omanga kama kiongozi aliyependa elimu na hakupoteza muda.
Katika kitabu chake Trails in Academic and Administrative Leadership, Michieka anaeleza kuwa Omanga alimpongeza kwa kazi nzuri aliyokuwa akifanya chuoni na papo hapo akampa barua ya kumteua kuwa mjumbe wa Bodi ya Bahari na Uvuvi ya Kenya ili kusaidia juhudi za kulinda mazingira ya pwani.
Mnamo Mei 1980, Omanga aliandika historia baada ya kuchukua likizo rasmi, hali iliyomlazimu Rais Moi kutumia mamlaka yake kuhamishia kwa muda majukumu yake kwa Waziri wa Maendeleo ya Maji Jonathan Ng’eno.
Mojawapo wa mambo yaliyotikisa kipindi chake serikalini lilihusu ufadhili wa Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Kenyatta (KICC).
Mwaka 1985, chama tawala cha KANU kiliamua kuwa KICC iwe sehemu ya mali yake pamoja na Kenya Times Media Trust na Press Trust Printing Company.
Hata hivyo, serikali iliendelea kufadhili shughuli za KICC kupitia Wizara ya Utalii.
Akizungumza bungeni Oktoba 9, 1986, Omanga alitetea hatua hiyo akisema kituo hicho kilikuwa muhimu kwa maendeleo ya utalii wa mikutano.
Alikumbusha wabunge kuwa KICC ilikuwa imeandaa mikutano mikubwa ya kimataifa kama ule wa Benki ya Dunia na Kongamano la Umoja wa Mataifa kuhusu Wanawake, ambalo lilitangaza Kenya duniani.
Alisema serikali ilinuia kuboresha KICC ili iweze kushindana na vituo vya kisasa vya mataifa kama Singapore.
Licha ya hayo, mwaka 1989 KANU ilichukua rasmi umiliki wa jengo hilo baada ya ardhi iliyokuwa imejengwa kuhamishiwa chama hicho.
Hatua hiyo ilifutwa mwaka 2003 kupitia amri ya Rais Mwai Kibaki.
Katika siasa za Gusii, Omanga pia alijikuta akipingana na aliyekuwa mlezi wake kisiasa, Simeon Nyachae.
Mwaka 1988 aliongoza kundi la wabunge wa eneo hilo kupinga azma ya Nyachae kugombea ubunge wa Nyaribari Chache.
Kupitia tamko lililojulikana kama Azimio la Kebirigo, walidai Nyachae alikuwa akinuia kutumia utajiri wake kufadhili wagombea dhidi yao.
Hatua hiyo ilichangia Nyachae kuzuiwa kushiriki uchaguzi mkuu wa mwaka huo.
Hata hivyo, baada ya kurejeshwa kwa mfumo wa vyama vingi mwaka 1992, Omanga alijiondoa kwenye kinyang’anyiro ili kumpisha Nyachae.
Mwaka 1993 aliteuliwa kuwa Mwenyekiti Mtendaji wa Shirika la Kenya National Assurance Corporation.
Omanga alifariki dunia mwaka 2004 akiwa na umri wa miaka 72.
Aliacha wake wawili, Clare na Grace, pamoja na watoto 10.
Baada ya kifo chake, Clare Omanga aliendelea na shughuli za maendeleo alizoanzisha mumewe na pia aliwahi kuwa diwani wa kuteuliwa.
Mwaka 1995 alikuwa sehemu ya ujumbe wa Kenya uliohudhuria Kongamano la Nne la Umoja wa Mataifa kuhusu Wanawake mjini Beijing, China.
Tofauti na wanasiasa wengine wa Gusii kama Nyachae, Zachary Onyonka na Lawrence Sagini, Omanga hakupenda kujitafutia umaarufu kupitia vyombo vya habari.
Badala yake alijikita katika miradi ya maendeleo mashinani.
Anakumbukwa kwa kujenga madarasa, majengo ya shule na miradi mingine ya kijamii katika eneo la Nyaribari kabla halijagawanywa.
Kabla ya kuingia katika siasa, Omanga alikuwa msomi aliyebobea.
Alisomea Shule ya Amasago na baadaye St Mary’s Nyabururu kabla ya kujiunga na Shule ya Upili ya Yala mwaka 1947.
Mwaka 1950 alihamia Shule ya Upili ya Mang’u.
Baadaye alisomea Shahada ya Sanaa katika Chuo Kikuu cha Makerere nchini Uganda, akibobea katika Kiingereza, Jiografia na Uchumi.
Mwaka 1956 alijiunga alienda mjini Bombay, India, alikopata Shahada ya Uzamili katika Sayansi ya Siasa.
Aliporejea Kenya aliajiriwa kama Meneja katika Kampuni ya East African Tobacco, ambayo sasa ni BAT.
Aliingia katika utumishi wa umma mwaka 1961 kama Katibu Msaidizi na mwaka 1966 Rais Jomo Kenyatta akamteua kuwa Katibu Mkuu katika Ofisi ya Makamu wa Rais na Wizara ya Masuala ya Ndani, hatua iliyofungua njia ya safari yake ndefu katika siasa za Kenya.