Polisi wajivuta kutoa kanda za CCTV kuhusu kesi ya wizi wa mabavu Nakuru
POLISI bado hawajatoa kanda ya CCTV kutoka kituo cha polisi cha Nakuru Central ambayo ilinaswa kwenye dawati la kuripoti matukio mnamo Juni 15, kuhususiana na kesi ya wizi wa kutumia nguvu inayowahusisha maafisa katika kituo hicho.
Bw David Ng’ang’a, mwenye umri wa miaka 37 na mwendeshaji wa bodaboda, alivamiwa na mteja aliyemuomba kumsafirisha kutoka katikati ya jiji hadi eneo la Milimani. Wakiwa njiani, mteja huyo alijiunga na wanaume wawili zaidi waliomnyang’anya pikipiki, simu, na pesa.
Katika harakati za kufuatilia kesi hiyo, Bw Ng’ang’a alisema alishangaa alipomuona mmoja wa wavamizi wake akihudumu kwenye dawati la kuripoti matukio ndani ya kituo hicho cha polisi, huku mwingine akiwa nje, wote wakiwa wamevalia sare za polisi.
Kulingana na Afisa wa Upelelezi wa Jinai wa Kaunti ya Nakuru, Bw Samuel Ngeiywo, maafisa wa upelelezi bado hawajapata kanda ya CCTV ya kituo hicho ambayo ni muhimu kwa kuwatambua maafisa waliodaiwa kuhusika.
Alisema ucheleweshaji huo umetokana na kutokuwepo kazini kwa Kamanda wa Polisi wa Kaunti, Bw Michael Mwaura, ambaye ndiye msimamizi wa CCTV na kumbukumbu za kituo hicho.
Bw Ngeiywo alisema kuwa wapelelezi tayari wamekagua kanda ya CCTV kutoka kwa biashara jirani ambayo ilimnasa Bw Ng’ang’a akimbeba mteja, lakini video hiyo haikuwa wazi kiasi cha kusaidia kutambua sura za washukiwa.
“Hatuwezi kutegemea kanda moja ya CCTV. Tuko mbioni kupata kanda kutoka ofisi ya kamanda na tunatarajia kuipata kabla ya mwisho wa wiki. Wapelelezi pia wametembelea boma la msamaria mwema aliyemsaidia Bw Ng’ang’a baada ya kuvamiwa, kusaidia katika uchunguzi,” alisema.
Kulingana na Bw Ng’ang’a, mnamo Juni 13 saa mbili na dakika 40 usiku, mteja mmoja alimkaribia baada ya kutoka katika baa moja mjini Nakuru na kumuomba ampeleke Milimani kuchukua kifurushi, kisha warudi mjini.
Mteja huyo, aliyekuwa akizungumza kwa simu, alimkabidhi Bw Ng’ang’a simu azungumze na mtu mwingine aliyekuwa atoe maelekezo zaidi. Baada ya majadiliano, walikubaliana bei ya Sh 200.
Hata hivyo, walipofika eneo walilokubaliana, mteja huyo alikutana na mwanamume mwingine, kisha wote wakamgeukia Bw Ng’ang’a. Mwanamume wa tatu aliyekuwa amejificha katika jengo la ujenzi lililoachwa, alijitokeza akiwa amebeba panga.
Wanaume hao watatu walimvuta hadi kichakani, wakamwamuru alale chini, kisha wakaanza kumpiga. Walimfunga mikono na miguu, na baada ya kuomba wasimuue, wakamziba mdomo.
Baada ya kumshika mateka kwa zaidi ya saa moja, wavamizi hao walitoroka na pikipiki yake, simu ya mkononi, na Sh 50 alizokuwa nazo mfukoni.
Hatimaye, aliweza kujifungua na kutafuta msaada katika maboma iliyokuwa karibu.