Amelewa mamlaka?
KAULI ya Waziri wa Usalama wa Ndani Kipchumba Murkomen Alhamisi kuwa polisi wawapige risasi wale ambao wanakaribia kituo cha polisi imeibua mdahalo mkubwa huku ikifasiriwa kama ya kuwapa ruhusu maafisa hao wa usalama kutekeleza mauaji kiholela dhidi ya Wakenya.
Bw Murkomen alitoa matamshi hayo huku taifa bado likiendelea kukadiria hasara kutokana na maafa, uporaji na majeraha yaliyotokea wakati wa maandamano ya Jumatano.
Maandamano haya yalikuwa ya kuwaenzi kizazi cha vijana cha Gen Z ambao waliaga dunia mwaka jana wakipinga Mswada wa Fedha 2024.
“Tunawaambia polisi kuwa mtu yeyote ambaye atakaribia kituo cha polisi, piga yeye risasi,” akasema waziri huyo
“Mtu yeyote ambaye amekuja kituo cha polisi kuchukua bunduki, anataka kuchukua afisi ya serikali, anatishia maisha yako, pita na yeye,” akaongeza Murkomen akikagua uharibifu uliotokea baada ya maandamano ya Jumatano jijini Nairobi.
Alizomewa na wananchi alipokuwa akitoa kauli hiyo walikwepo wakipendekeza watu wanaopambana na polisi washikwe na kupelekwa mahakamani.
“Ashikwe, asiuawawe wacha wewe,” baadhi ya wananchi wakasikika wakimzomea Bw Murkomen.
Waziri huyo alifafanua kuwa polisi hawafai kuwalenga wale wanaokuja kuandikisha ripoti kituoni au msaada wowote ule bali wanaowadhuru maafisa wa usalama.
“Hiyo kesi nyingine mimi nitashughulikia, bora hujatoka hapa kuenda kuua mtu nje. Mtu amekuja kituoni anataka bunduki, usikubali upigwe kama askari hata kama ni madharau kwa polisi. Fanya kabisa yenye utaweza, tutafanya kesi hiyo nyingine baadaye,” akasema Bw Murkomen.
Katika maandamano ya mnamo Jumatano kulikuwa na visa vya waandamanaji kuvamia vituo vya polisi na kuviteketeza huku baadhi ya maafisa wakijeruhiwa.
Tukio la hivi punde lilikuwa mnamo Alhamisi jioni ambapo kituo cha polisi kiliteketezwa Ndunyu, Kaunti ya Nyandarua.
Kituo hicho kilichomwa baada ya polisi kumpiga risasi mwanakijiji ambaye alikuwa sehemu ya umati uliokuwa ukilenga kuwateketeza wezi wa mifugo waliokuwa wakizuiliwa kituoni humo.
Kwa mujibu wa Sheria ya Tume ya Huduma kwa Polisi (NPS) polisi anaruhusiwa kuua anapolinda maisha yake au maisha ya mtu mwengine dhidi ya kukatizwa.
Hata hivyo, sheria hiyo inawataka polisi wafanye kila juhudi kuzuia kutumia bunduki hasa dhidi ya watoto.
Pia wengi wameuliza jinsi polisi atakavyokimbilia kumuua aliyejihami na silaha kama mawe ilhali afisa wa usalama ana uwezo wa kumnyaka kisha mkondo wa sheria ufuatwe.
Kauli ya Bw Murkomen japo imesukumwa na uharibifu ambao ulitokea wakati wa maandamano Jumatano, huenda ukawashaajisha polisi kutekeleza dhuluma zaidi dhidi ya raia, kwa mujibu wa baadhi ya Wakenya.
Bw Murkomen pia alieleza kuhangaishwa kwake na mchakato wa utekelezaji wa sheria mahakamani ambayo pia inawaruhusu watu ambao wameshiriki uhalifu kuachiliwa kwa dhamana ya polisi.
“Wanawaachiliwa kwa dhamana ya chini na kurejea kupambana na polisi na hata kuwadhihaki. Hiyo lazima ikomeshwe,” akasema.
Mwenyekiti wa Chama cha Mawakili Nchini (LSK) Faith Odhiambo alisema agizo la Bw Murkomen ni haramu na kuwaonya maafisa wa polisi dhidi ya kutekeleza mauaji.
“Waziri wa Usalama wa Ndani kisheria hana mamlaka ya kutoa amri kama hiyo. Afisa yeyote wa usalama atakayeua kwa msingi wa kutekeleza amri ya Murkomen atabeba msalaba wake mwenyewe,” ikasema taarifa ya Bi Odhiambo.
Rais huyo wa LSK alimtaka Inspekta Jenerali wa Polisi Douglas Kanja aingilie kati ili amri aliyosema ni haramu kama ya Bw Murkomen
Mbunge wa Kipipiri Wanjiku Muhia alishutumu amri ya Bw Murkomen akisema kuwa inaweza kufasiriwa vibaya na polisi ambao watawaua Wakenya wanaosaka haki zao.
“Kusema yeyote anayetembelea polisi apigwe inaonyesha hulewi chochote kuhusu sheria. Vituo vya polisi si vyako, wewe tu ni waziri na siku moja utatoka,” akasema Bi Muhia akiwahutubia wanahabari katika majengo ya bunge.
Seneta wa Murangá Joe Nyutu naye alisema vituo vya polisi ni asasi za umma wala si vya kuwapiga watu risasi.
“Sote tunajua jinsi ambavyo masuala ya usalama huchukuliwa nchi na matamashi ya Murkomen yanaonyesha kuwa utawala huu unalenga kuwadhuru Wakenya wanaopigania haki zao,” akasema pia Bw Nyutu katika majengo ya bunge.
Kauli aliyoyatoa Bw Murkomen inaongeza matamshi tata ambayo yamekuwa yakimwaandama tangu achukue usukani kwenye wizara hiyo baada ya Profesa Kithure Kindiki aliyeteuliwa naibu rais.
Hasa waziri huyo amekuwa akilaumiwa kwa utendakazi duni kutokana na kupanda kwa visa vya mauaji ukanda wa Kaskazini mwa Bonde la Ufa ambako raia wamekuwa wakiteseka mikononi mwa majangili.
Hata hivyo, mwezi uliopita alikanusha hilo akisema kuwa visa vya ujangili eneo hilo vilikuwa vimepungua kwa miezi mitano ambayo amekuwa kwenye wizara hiyo.
“Mkiniona nakaa mtu wa kucheza na mambo ya ujangili? Sahau kuhusu hizi taarifa zinachapishwa na wanahabari, tupeeni takwimu na idadi,
“Nimekuwa waziri wa usalama kwa miezi mitano nimepunguza ujangili na sio eti nataka nisifiwe, kuna maafisa wa usalama ambao wamefanya kazi hiyo,” akasema Bw Murkomen.
Aidha vifo ambavyo vimekuwa vikitokea vya Wakenya kwenye vituo vya polisi vimetia doa utendakazi wa waziri huyo.
Kuuawa kwa bloga na mwalimu Albert Ojwang’ mikononi mwa polisi na hata Naibu Inspekta Jenerali wa Polisi Eliud Lagat kutajwa kama mlalamishi, kumeipaka tope zaidi utendakazi wa Bw Murkomen.