David Ketter apandishwa cheo, sasa kusimamia Jeshi la Nchi Kavu
RAIS William Ruto jana aliwateua makamanda wapya wa Jeshi na Kikosi cha Jeshi la wana Anga kisha kuwaidhinisha maafisa 21 wapandishwe vyeo katika huduma ya jeshi.
Mabadiliko hayo yalitangazwa kufuatia mapendekezo kutoka kwa Baraza la Ulinzi ambalo ni taasisi ya juu zaidi ya kufanya maamuzi yanayohusu Jeshi la Ulinzi Nchini (KDF).
Meja Jenerali David Kipkemboi Ketter alipandishwa cheo kuwa Luteni Jenerali na kuteuliwa Kamanda wa Jeshi la Nchi Kavu.
Ni hatua kuu kwa taaluma ya Luteni Jenerali Ketter katika KDF kwa kuwa 2023 alikuwa miongoni mwa maafisa wa jeshi waliotunukiwa na rais. Wakati huo alipandishwa cheo na kuteuliwa kuwa Naibu Kamanda wa Jeshi la Nchi Kavu.
Luteni Jenerali Ketter amechukua nafasi ya Luteni Jenerali David Kimaiyo Chemwaina Tarus, ambaye amepelekwa katika Chuo Kikuu cha Ulinzi Kenya ili kuhudumu kama naibu chansela.
Hadi uteuzi wake mpya, Luteni Jenerali Ketter alihudumu vilevile kama Naibu Mkuu wa Vikosi vya Ulinzi aliyesimamia wafanyakazi na mipangilio.
Hatua ya kumtaja Luteni Jenerali Ketter kama Mkuu wa Jeshi la Nchi Kavu ina maana ndiye mtu wa tatu kwenye foleni ya kuwa mkuu wa jeshi nchini. Hii ni kwa kufuata mzunguko wa kuyatoa mamlaka kwenye uteuzi wa mkuu wa jeshi, kulingana na sheria zilizowekwa na Jenerali Mstaafu Daudi Tonje.
Wengine katika daraja hilo ni pamoja na Luteni Jenerali Tarus na Luteni Jenerali Juma Shee Mwinyikai (Kamanda wa Chuo cha Kitaifa kuhusu Mafunzo ya Ulinzi).
Uteuzi wa kuwa mkuu wa jeshi nchini, hata hivyo, unazingatia masuala mengine, ukiwemo umri.
Jenerali Charles Kahariri anatoka kikosi cha jeshi la wanamaji naye Jenerali Francis Ogolla aliyeaga dunia Aprili mwaka jana, alitoka kikosi cha Jeshi la Anga.