Ruto aunga Murkomen wanaharakati wakinyakwa
RAIS William Ruto ameagiza msako wa kitaifa dhidi ya watu aliotaja kama “waliochochea wahuni” waliotekeleza uharibifu wa mali wakati wa maandamano ya Juni 25, huku akiapa kutoa ulinzi kamili kwa maafisa wa usalama wanaokabiliana na vurugu kote nchini.
Kiongozi huyo wa taifa aliunga mkono kauli ya Waziri wa Usalama wa Ndani Kipchumba Murkomen, akisema kuwa atasimama kidete kuwatetea maafisa wa usalama wanapotekeleza majukumu yao.
“Nitasimama na kila afisa. Nitajitahidi kuhakikisha hawatishiwi,” alisema Rais Ruto. “Watoto wao na familia zao lazima wawe salama—kwa sababu hio ndio njia pekee ya kuhakikisha familia zetu pia ziko salama.”
Alisema haya katika kikao cha wakuu wa usalama akiwemo Inspekta Jenerali wa Polisi Douglas Kanja, Mkurugenzi wa Upelelezi wa Jinai (DCI) Mohammed Amin, Naibu Inspekta Jenerali Gilbert Massengeli na Maafisa wa Utawala wa Kitaifa kutoka maeneo mbalimbali, kilichofanyika Ikulu chini ya uenyekiti wake pamoja na Bw Murkomen.
Rais Ruto alizungumza vikali, akitangaza mabadiliko makubwa katika jinsi serikali itakavyokabiliana na uhalifu na utovu wa nidhamu.
“Hatuwezi kuwa na nchi ambapo wahalifu wanawakimbiza polisi,” alisema. “Kama maisha ya polisi hayako salama, basi maisha ya nani yako salama?”
Kauli hiyo ya rais ilitolewa huku serikali ikiendelea na oparesheni kali dhidi ya watu wanaodaiwa kuhusishwa na ghasia wakati wa maandamano. DCI imetangaza kuwa watu 27 walikamatwa kwa tuhuma za uporaji, uchomaji mali, na uharibifu wa miundombinu ya serikali na binafsi.
Wengi wa waliokamatwa ni vijana wenye umri wa kati ya miaka 19 hadi 25.
Miongoni mwao ni wanaharakati wa haki za binadamu akiwemo John Mulingwa Nzau, Katibu Mkuu wa Chama cha Ukweli, Mark Amiani na Francis Mutunge Mwangi. Walikamatwa Jumamosi asubuhi wakiwa ndani ya basi lililokuwa linaelekea Mombasa, na wanazuiliwa katika Kituo cha Polisi cha Muthaiga wakisubiri kufikishwa mahakamani Jumatatu.
Kwa mujibu wa DCI, watu 25 kati ya waliokamatwa wanahusishwa moja kwa moja na kuchomwa kwa Mahakama ya Kikuyu, afisi za eneo dogo na magari ya serikali pamoja na ya kibinafsi.
Hata hivyo, kukamatwa kwao kumekosolewa vikali na wanaharakati wa haki za binadamu waliodai kuwa serikali inatumia hofu na vitisho kuwanyamazisha vijana.
“Tunataka serikali ikomeshe mara moja kukamatwa kiholela kwa waandalizi wa maandamano. Huu udhalimu hautazuia mapinduzi yanayokuja. Kutumia polisi kueneza hofu na kutisha wanaharakati wa jamii na watetezi wa haki za binadamu kutachochea hasira zaidi miongoni mwa umma,” ilisema Kongamano la Mapinduzi kupitia ukurasa wao wa X.
Inakadiriwa kuwa magari ya polisi takriban 80 yaliharibiwa au kuchomwa moto wakati wa maandamano, huku vituo kadhaa vya polisi vikivamiwa na sare pamoja na silaha kuibwa. Biashara kadhaa pia ziliripotiwa kuporwa maeneo tofauti nchini.
Rais Ruto aliahidi mwelekeo mpya na mkali wa sera za usalama, akizungumza katika hafla tofauti ya kuwaapisha makamanda wapya wa Jeshi la Nchi Kavu na Kikosi cha Anga. Alisema serikali itawaunga mkono kikamilifu.
“Tunapotekeleza majukumu ya kuilinda nchi yetu na kuhakikisha kuna utulivu na amani kwa wananchi kutekeleza shughuli zao, kwenda kazini, kuhudumu katika nyanja mbalimbali na kulinda familia na mali zetu—tunahitaji mfumo thabiti,” alisema.
Alisisitiza kuwa serikali itawekeza katika vifaa na mahitaji ya maafisa wa usalama walioko mstari wa mbele, akisema usalama wao ni msingi wa utulivu wa kitaifa.
“Ninataka kuwaambia kila afisa wa polisi anayeamka mapema kila siku na kujitolea kulinda watoto wetu, familia zetu na taifa letu—kuwa sisi kama serikali tumejizatiti kuhakikisha mnapata ulinzi ninyi, familia zenu, na watoto wenu,” alisema Rais Ruto.