Dimba

Okutoyi ajibwaga W35 Amstelveen baada ya kuangukia pua W15 Alkmaar

Na GEOFFREY ANENE June 29th, 2025 Kusoma ni dakika: 1

NYOTA Angella Okutoyi leo ataelekeza nguvu zake kwa mashindano ya tenisi ya malipo ya wanawake ya W35 Amstelveen nchini Uholanzi baada ya kubanduliwa katika W15 Alkmaar mnamo Ijumaa.

Bingwa huyo wa Michezo ya Afrika kitengo cha mchezaji mmoja kila upande alipoteza katika kitengo hicho kwa alama 6-3, 1-6, 3-6 mikononi mwa Mjerumani Fabienne Gettwart mechi ya robo-fainali.

Saa chache baadaye Okutoyi akishirikiana na Mjerumani Gina Marie Dittmann walizidiwa maarifa na Waholanzi Loes Ebeling Koning na Sarah Van Emst katika nusu-fainali ya wachezaji wawili kila upande.

Kabla matokeo hayo Okutoyi alikuwa amefika fainali katika vitengo hivyo viwili kwenye mashindano ya W15 Bolszewo nchini Poland. Alisalimu amri ya Amelie Van Impe 6-7, 6-0, 2-6 kitengo cha mchezaji mmoja kila upande.

Vile vile, alipoteza dhidi ya Rikke De Koning (Uholanzi)/Amelie Van Impe alama 7-6, 3-6, 10-7 akishirikiana na Salma Drugdova wa Slovakia katika kitengo cha wachezaji wawili.

Wakati huo huo, hii leo Mkenya Kael Shah pia atafungua kampeni yake ya mashindano ya M15 Monastir nchini Tunisia ambayo yanahusisha wanaume pekee.