Maoni

MAONI: Dhuluma za kimapenzi zipo kazini ila kunao wanaojipeleka kichinjioni

Na PAULINE ONGAJI June 30th, 2025 Kusoma ni dakika: 1

KUMEKUWA na mjadala mkali kuhusu dhuluma za kimapenzi katika maeneo ya kazini.

Suala tata limekuwa jinsi ya kutofautisha kati ya dhuluma za kimapenzi, na shutuma ibuka zinazojiri baada ya penzi la watu wawili wakomavu na waliosikizana, kugeuka na kuwa shubiri.

Dhuluma za kimapenzi kazini hutokea hasa mhusika anapotumia mamlaka yake na kumlazimu mwenziwe kujihusisha naye katika uhusiano wa kimapenzi.

Kwa upande mwingine, penzi la kazini kugeuka kuwa shubiri huwa ikiwa wahusika wote wanapokubaliana kuingia katika uhusiano wa kimapenzi, lakini muda unavyosonga, mmoja (ambaye hasa huwa mwenye mamlaka ya juu) anamtema mwenziwe.

Hili ni suala ambalo kwa sababu moja au nyingine huwaathiri hasa wanawake.

Lakini tuambianeni ukweli.

Mara nyingi mabinti wanaoingia katika mahusiano na wakubwa wao kazini bila kushurutishwa, hufanya hivyo wakiwa na nia ya kunufaika katika mazingira ya kikazi.

Lakini habari mbaya ni kwamba wengi wao huishia kujuta wanapotemwa, kwani uhalisi wa maisha ni kwamba madume wa aina hii kazini huwa na mazoea kuonjaonja maji ya visima tofauti kabla ya kutoweka.

Inapofikia hapa basi ndipo mambo huharibika na siri zilizokuwa zikifichwa kuwekwa hadharani.

Hapa ndipo utaanza kusoma kuhusu madai ya dhuluma za kimapenzi mitandaoni, au hata uvumi kurushwa huku na kule huku wahusika wakitaka kuonewa huruma.

Nasisitiza kwamba kunao madume katika mazingira ya kazi wanaotumia mamlaka yao kushurutisha mabinti kulala nao, lakini uhalisi wa mambo ni kwamba katika baadhi ya visa, mabinti wahusika hufanya hivyo bila kulazimishwa.

Na wengi wanaofanya hivi hujitokeza wakati tu biashara yao ya kuuza minofu inapodidimia.

Kinachoudhi hata zaidi ni kwamba katika kipindi cha mahusiano ya aina hii, mabinti wengi wa aina hii hufanya kila wawezalo kurejesha wenzao nyuma.

Hawa ndio mabinti wanaotatiza wanawake wenzao wanaotia bidii kazini, kuhakikisha kwamba hawasongi kitaaluma.

Hawa ndio mabinti wanaotumia mahusiano haya kuwapokonya wenzao kazini fursa za kupokea wanachostahili kutokana na bidii yao.