Michezo

Ngetich akosa rekodi ya dunia na Sh10.4M kwa sababu ya upepo mkali

Na GEOFFREY ANENE October 27th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

UPEPO umemnyima Agnes Jebet Ngetich rekodi ya dunia na bonasi ya Sh10.4 milioni mwanadada huyo akiibuka malkia wa Valencia Half Marathon tena nchini Uhispania, Jumapili, Oktoba 26, 2025.

Mkenya huyo amekosa rekodi ya dunia ya mbio hizo za kilomita 21 kwa sekunde 16 baada ya upepo mkali kutoka mbele kumnyima fursa hiyo.

Licha ya upepo mkali katika kilomita za mwisho, Ngetich alimaliza umbali huo kwa saa 1:03:08, muda ambao ni bora zaidi kwa mwaka huu na wa tatu kwa kasi katika historia.

Mshikilizi huyo wa rekodi ya dunia ya 10km, ametia kibindoni Sh5.2 milioni kwa kunyakua taji chini ya dakika 65.

Ngetich alikuwa akikimbia kwa mwendo wa kuvunja rekodi ya dunia ya Muethiopia Letesenbet Gidey ya 1:02:52 iliyowekwa Valencia Half Marathon mwaka 2021, lakini hali ya hewa ilimzuia kufikia lengo hilo.

Fotyen Tesfay kutoka Ethiopia alimaliza wa pili kwa 1:05:10 na kutuzwa Sh2.6m, huku Mkenya Veronica Loleo akifunga tatu-bora kwa 1:05:46 na kuvuna Sh749,000.

Katika 21km za wanaume, Muethiopia Yomif Kejelcha pia alitetea ubingwa wake akikata utepe kwa dakika 58:02. Kejelcha alilenga kuboresha rekodi yake ya dunia ya mwaka 2024 ya 57:30, lakini hali mbaya ya anga ilimlazimu kupunguza kasi. Rodrigue Kwizera kutoka Burundi aliridhika na nafasi ya pili kwa 58:38, akifuatwa kwa karibu na Mkenya Brian Kibor aliyemaliza kwa 58:39. Yomif alipata Sh5.2m, Kwizera Sh2.6m naye Kibor Sh1.4m.

Mswidi Andreas Almgren hakutetemeshwa na upepo mkali na akaweka historia kwa kuvunja rekodi ya Ulaya akimaliza katika nafasi ya nne kwa 58:41.

Kwa upande wa taifa la Uhispania, Carlos Mayo alishinda taji la wanaume kwa saa 1:00:46. Ingawa muda huo uko mbali na rekodi yake ya Uhispania ya 59:39, Mayo anaendelea kujikita katika maandalizi ya Valencia Marathon itakayofanyika Desemba 7. Kwa upande wa wanawake wa Uhispania, ushindi ulienda kwa Carla Gallardo (1:09:14). Bonasi ya Sh10.4m (Yuro70,000) ilikuwa imewekwa mezani kwa yeyote angepata rekodi ya dunia.

Matokeo (10-bora):

Wanawake:

Agnes Jebet Ngetich saa 1:03:08

Fotyen Tesfay 1:05:11

Veronic Loleo 1:05:46

Gladys Chepkurui 1:06:58

Mulat Tekle 1:07:08

Emma Hurley 1:08:02

Klara Lukan 1:08:04

Alessia Zarbo 1:08:20

Caroline Nyaga 1:08:40

Carla Gallardo Puebla 1:09:14

Wanaume:

Yomif Kejelcha dakika 58:02

Rodrigue Kwizera 58:39

Brian Kibor 58:39

Andreas Almgren 58:41

Adriaan Wildschutt 59:13

Nicholas Kipkorir 59:44

Mohamed Ismail saa 1:00:03

Gideon Kiprotich 1:00:03

Filmon Tesfu 1:00:46

Carlos Mayo 1:00:47