Hali tete Afrika Kusini maandamano ya kuwafukuza wageni yakiandaliwa
HALI inatarajiwa kuwa tete Afrika Kusini huku raia wa mataifa mbalimbali wakiharakisha kuondoka nchini humo kutokana na maandamano makubwa yanayotarajiwa Jumanne, Juni 30, 2026.
Maandamano hayo yatafanywa na raia wa Afrika Kusini ambao wamekuwa wakiendeleza wito wa kuwafurusha raia wa kigeni nchini humo.
Kesho ndiyo makataa ya raia wa kigeni wasiokuwa na stakabadhi halali kuondoka Afrika Kusini ambako wamelaumiwa kwa kutwaa nafasi za ajira na kusababisha raia wa taifa hilo mahangaiko makubwa.
Jumatatu, maelfu ya wahamiaji kutoka Malawi walijipanga kwenye foleni katika kambi ya muda jijini Durban, wakisubiri kushughulikiwa ili warejee kwao.
Nao mamia ya raia wa Zimbabwe walilala kando ya barabara nje ya ubalozi wao mjini Cape Town wakiharakisha kuondoka kabla ya maandamano ya Jumanne.
Raia wengi wa kigeni wanahofia kuwa maandamano hayo yataishia kwenye ghasia huku hasira dhidi ya wahamiaji zikiendelea kuongezeka miongoni mwa wenyeji.
“Tuna hofu kwa sababu huwezi kujua watu wanapanga kukufanyia nini tunasubiri kuona tu kitakachotokea,” akasema Ebrahim Moosa, 37.
Alikuwa pamoja na mkewe katika foleni ndefu ya watu, baadhi yao wakiwa wamewabeba watoto migongoni, wakitarajia kupata basi la kuelekea Malawi kutoka Durban.
Makundi yanayopinga wahamiaji yaliweka Juni 30 kama siku ya mwisho ya wahamiaji wote wasio na stakabadhi halali kuondoka Afrika Kusini.
Serikali ya Rais Cyril Ramaphosa nayo imeonekana kuwa vuguvugu kuhusu suala hilo japo imewataka raia wasichukue sheria mikononi mwao.
“Tunawasihi wote watakaoshiriki katika maandamano kuheshimu polisi,” akasema Phumelele Makoba, kaimu kamishna wa polisi wa mkoa wa KwaZulu-Natal.
Mkoa huo ni kati ya maeneo ambayo mvutano mkubwa unatarajiwa kati ya raia na maafisa wa usalama.
“Vyombo vyetu vya usalama viko tayari kukabiliana na machafuko yoyote,” akasema Rais Ramaphosa.
Kiongozi huyo kwa kipindi kimoja aliwalaumu raia akisema kuwa hawafai kuwabebesha wageni lawama zote kwa sababu ubaguzi wa rangi maarufu kama apartheid ndio chimbuko la changamoto zote Afrika Kusini.
Licha ya changamoto kadhaa, Afrika Kusini ndiyo ina uchumi mkubwa zaidi Afrika na huvutia watu wanaotafuta ajira kutoka mataifa mengine.
Antonio Njive kutoka Msumbiji, ambaye amekuwa akifanya vibarua nchini Afrika Kusini tangu 2019, aliondoka Juni 1 baada ya nyumba yake kuchomwa moto.
“Niliondoka nyumbani bila hata nguo. Kila kitu kiliteketea kwa moto,” akasema kwa simu akiwa Chibuto, Msumbiji.
Njive, mkewe na binti yao mwenye umri wa miaka sita walikuwa miongoni mwa mamia ya raia waliorejeshwa kwao kupitia uchukuzi wa mabasi na serikali ya Msumbiji.