Maoni

Usimtishie mbunge wako bila vitendo, jisajili kupiga kura

Na DOUGLAS MUTUA February 2nd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

ACHA kumtishia mbunge wako kwamba hatarejea Bungeni baada ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka kesho, unda mikakati ya kuhakikisha harudi.

Hilo la kutorudi si tishio, analifahamu fika, na ndiyo maana anaendelea kujiandalia chochote ambacho kinaweza kutokea ukimfuta kazi.

Vitisho vyako si vigeni, tayari amekwisha kuambiwa na Spika Moses Wetang’ula kwamba takwimu zinaonyesha asilimia 56 ya wabunge wa sasa hawataona ndani ya Bunge baada ya uchaguzi ujao.

Na kila mbunge anajua katika kilindi cha moyo wake iwapo yeye yuko katika asilimia ya watakaotemwa au watakaosazwa; wanasiasa ni wajanja, huwa wanajua vyema jinsi uhusiano mbaya kati yao na wananchi unavyoweza kuwaathiri.

Kauli hiyo ya Bw Wetang’ula inanikumbusha nyingine ya kijeuri iliyotolewa na Mbunge wa Kikuyu, Bw Kimani Ichung’wa, baada ya wakazi wa Mlima Kenya kupaza sauti na kuwatishia wabunge wao waliofungamana na serikali ya Rais William Ruto mwishoni mwa mwaka 2024.

Ilikuwa ni baada ya kutimuliwa kwa Bw Rigathi Gachagua kama naibu rais ambapo wakazi hao walikuja juu na kuapa kwamba mbunge yeyote wa eneo lao aliyeunga mkono hatua hiyo ‘atakwenda nyumbani ifikapo mwaka 2027’.

Bw Ichung’wa, akionekana wazi kuchushwa na vitisho hivyo, aliwaambia wakazi kwamba wamkome pamoja na wabunge wengine kwa kuwa ‘sisi huenda nyumbani kila siku baada ya kazi’.

Dah! Mlimani palichimbika kweli baada ya Bw Gachagua kutimuliwa. Nakumbuka wabunge kadha wa eneo hilo waliopiga kura kumtimua wakifukuzwa baa kwa kuambiwa ‘muthuri nduinuke kama uhurwo…’ (mzee nenda nyumbani au upigwe).

Mpaka leo watu wakikosana hutishiana hivyo huko!

Kauli nyingine ambayo nilikumbuka baada ya tahadhari hiyo ya Bw Wetang’ula ikitolewa mwishoni mwa miaka wa tisini na aliyekuwa mbunge wa mwala, Bw Mutua Katuku, baada ya wakazi kumshinikiza awatimizie mahitaji yao kwa kuwa angalihitaji kura zao.

Huyo naye akiwakomesha kwa kuwaambia waache vitisho, eti hakuwa amemwambia yeyote kwamba angalitetea kiti chake cha ubunge wakati wa uchaguzi uliofuata.

Binafsi nilikomeshwa kwa namna fulani na mbunge mteule wa Jubilee, Bi Sabina Chege, niliposhiriki mdahalo naye katika mojawapo ya runinga siku chache kabla ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2022.

Nilimkasirisha kwa kumwambia kuwa yeye na wabunge wenzake walipaswa kuanza kufunganya virago ili kuondoka Bungeni kwa kuwa ilitabiriwa asilimia zaidi ya 50 ya wabunge hawangechaguliwa tena.

Alinikosoa kwa kuniambia kuwa, kikawaida, historia ilionyesha asilimia 75 ya wabunge huwa hawachaguliwi tena, hivyo takwimu zangu hizo zilikuwa chini, niliyotamka hayakuwa mageni mjini.

Spika Wetang’ula aliwapa wabunge takwimu hizo ili kuwashawishi kuunga mkono mswada unaolenga kuwakinga na masaibu ya kustaafu, hasa kwa kuwapa bima endelevu ya afya na mafao bora ya uzeeni.

Badala ya kumtishia mbunge wako kwamba hutamchagua tena, jiandikishe kupiga kura na uhakikishe hujamchagua kwa sababu tayari serikali imempangia maisha bora ya baada ya kustaafu. Vitisho vyako havisaidii kitu ikiwa hujajiandikisha kupiga kura.

Aliposema baadhi yao hawataona ndani ya Bunge alinikumbusha kisa cha mbunge fulani aliyetokea eneo la Mbooni ambaye, baada ya kustaafu, mambo yalimwendea vibaya hivi kwamba aligeuka omba-omba.

Bila shaka wabunge wengi wa sasa ni wafanyabiashara matajiri na wana taaluma mbalimbali zinazoweza kuwaingizia kipato hata baada ya kushindwa chaguzini, lakini ni hulka ya binadamu kuogopa kutumbukia ndani ya lindi la umaskini tena akishaondokana nao.

Na ndiyo maana naamini wataichukulia kauli ya Spika Wetang’ula kwa uzito unaostahili ili wajikinge na hali yoyote inayoweza kuwarudisha nyuma, waishi maisha ya ukata kama wanayoishi asilimia zaidi ya 90 ya waliowachagua.

Kenya ni mojawapo wa mataifa yasiyo ya usawa wa kijamii na kiuchumi hata kidogo; pengo kati ya maskini na matajiri linaendelea kupanuka, na hakuna anayeonekana kujali kitu.

Mbona wabunge wa sasa na waliostaafu wanahitaji bima maalum ya afya badala ya ile ya kitaifa ya SHA?

– Douglas Mutua ni mwanahabari Mkenya anayeishi Amerika (mutua_muema@yahoo.com)