Sifuna sasa alenga kusajili Linda Mwananchi
SENETA wa Nairobi Edwin Sifuna ameanza mchakato wa kusajili Linda Mwananchi kuwa chama cha kisiasa atakachotumia kuwania urais mnamo 2027.
Washirika wa Bw Sifuna wamethibitisha kuwa tayari wameweka mikakati mbadala iwapo juhudi hizo zitakumbana na vikwazo vya kisheria au kisiasa.
Viongozi wa mrengo wa Linda Mwananchi, ambao ni mrengo wa waasi ndani ya ODM, walisema wamepanga kukutana na Afisi ya Msajili wa Vyama vya Kisiasa (ORPP) leo ili kuendeleza mchakato wa kusajiliwa kwa chama hicho.
Baadhi yao walidai kuwa tayari wamehifadhi jina hilo, ingawa haikubainika iwapo liliidhinishwa kama lilivyo au kufanyiwa marekebisho.
Hatua ya sasa inafuatia ombi la awali la kusajili chama kwa jina Linda Mwananchi Party of Kenya (LMPK) kukataliwa na Msajili wa Vyama vya Kisiasa, John Cox Lorionokou.
Katika barua yake kwa Charles Wanyonyi aliyewasilisha ombi hilo, msajili alisema jina hilo linafanana na kaulimbiu nyingine zilizohifadhiwa, ikiwemo Linda Mkenya na Boresha Kenya, hivyo haliwezi kuidhinishwa kwa mujibu wa Sheria ya Vyama vya Kisiasa.
Hata hivyo, viongozi wa Linda Mwananchi wanasema hawajakata tamaa. Seneta wa Kisii Richard Onyonka alisema wameandaa majina mengine mawili mbadala iwapo usajili wa jina hilo utakwama.
“Jumatatu tunakutana na Msajili wa Vyama vya Kisiasa. Tayari tumeshahifadhi jina hilo, lakini katika siasa za Kenya ni lazima uwe na mpango B na C. Tumejipanga kwa sababu tunaamini ODM imekufa kisiasa,” akasema Bw Onyonka.
Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi alisema hakuna mtu anayeweza kuwazuia kusajili chama hicho kwa jina la Linda Mwananchi kwa kuwa tayari limejulikana kitaifa kama utambulisho wa mrengo wao.
“Linda Mwananchi ni yetu. Ndilo jina ambalo wananchi wanalitambua, na hakuna atakayetuzuia kulitumia,” akasema Bw Osotsi.
Aliongeza kuwa tayari wameunda jopo la wataalamu litakalotayarisha katiba, sera na ilani ya chama hicho kabla ya uchaguzi mkuu wa 2027.
Ingawa mbunge wa Suba Kusini Caroli Omondi analiwakilisha kundi hilo katika Baraza la Azimio, Bw Osotsi alisema kipaumbele chao kwa sasa ni kusajili chama na kukijenga nchini kote kabla ya kuingia katika mazungumzo ya miungano ya kisiasa.
“Hatua ya kwanza ni kuwa na chama na kukieneza katika kaunti zote 47. Baada ya hapo tutaanza mazungumzo ya kuunda muungano mkubwa wa upinzani,” alisema.
Hatua hiyo inajiri wakati Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta ameanza kuweka juhudi mpya za kuunganisha vyama vya upinzani ili viweze kumenyana na Rais William Ruto katika uchaguzi wa 2027.
Bw Onyonka na Bw Osotsi walisisitiza kuwa Bw Sifuna ndiye mgombea wao wa urais na watashawishi vyama vingine vya upinzani kumuunga mkono.
Mbunge wa Kitutu Chache Kusini Anthony Kibagendi naye amesema Linda Mwananchi itaungana na vyama vingine katika muungano mkubwa wa upinzani.
“Njia pekee ya kumshinda Rais Ruto ni vyama vya upinzani kuungana na kumsimamisha mgombeaji mmoja,” akasema Bw Kibagendi.
Mkutano wa Azimio unatarajiwa kujadili mfumo wa kuwasimamisha wagombea wa pamoja huku ukihusisha vyama vya Wiper, Jubilee, Kanu na vingine pamoja na makundi mapya kama Linda Mwananchi, DCP ya aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua na People’s Liberation Party (PLP) ya Martha Karua.
Wachanganuzi wa siasa wanasema historia imeonyesha kuwa mgawanyiko wa upinzani umekuwa ukiwanufaisha walio madarakani.
Mnamo 1992 na 1997, upinzani ulishindwa kumwondoa aliyekuwa Rais Daniel arap Moi kutokana na kusimamisha wagombea wengi wa urais.
Hali kama hiyo ilijitokeza mnamo 2007, ambapo mgawanyiko kati ya Raila Odinga na Kalonzo Musyoka uliigawa kambi ya ODM na kumwezesha Rais Mwai Kibaki kutangazwa mshindi katika uchaguzi uliosababisha machafuko makubwa baada ya matokeo kutangazwa.
Kwa sasa, viongozi wa Linda Mwananchi wanaamini kuwa chama kipya kitakuwa msingi wa kuunganisha upinzani na kumpa Bw Sifuna jukwaa la kuwania urais 2027.