Wakulima wanavyoweza kuzalisha chakula licha ya ukame unaoshuhudiwa
MWAKA huu wa 2026 umeanza kwa ukame katika maeneo mengi ya nchi, hasa sehemu kame na nusu kame (ASAL).
Kaunti zisizopungua 10, kulingana na Serikali na Mamlaka ya Kuangazia Majanga (NDMA), zimeathirika pakubwa huku zaidi ya watu milioni 2 wakikabiliwa na baa la njaa.
Mandera, Turkana, Wajir, na Marsabit, zimeandikisha upungufu mkubwa wa maji na chakula hasusan cha mifugo.
Ukame na kiangazi kinachoshuhudiwa sehemu tofauti nchini, ni kutokana na kiwango cha chini cha mvua iliyokunya kati ya Oktoba na Desemba 2025.
Kwa wakulima wa mashamba madogo, hali hii inaleta wasiwasi mkubwa kuhusu uzalishaji wa chakula.

Lakini kulingana na wataalamu wa masuala ya kilimo, suluhu ipo ikiwa wakulima watakumbatia mifumo ya kuvuna maji misimu ya mvua na kuwekeza kwenye teknolojia za kunyunyizia mimea na mashamba maji kwa kutumia mifereji.
“Hatua ya kwanza kabisa ni kuhakikisha usalama wa maji,” anasema Richard Omondi, mwasisi na mmiliki wa kampuni ya Agri-Irrigation and Solutions Africa, inayotoa huduma na ushauri wa mifumo ya kisasa kumwagilia mashamba na mimea maji.
Kampuni hiyo pia huchimba visima na mabwawa.
Mtaalamu Omondi anasisitiza kwamba uwepo wa maji ndiyo nguzo kuu kuhakikisha suala la njaa linaangaziwa.

“Maji ndiyo kikwazo kikubwa zaidi katika uzalishaji wa chakula. Bila maji, hata mbegu bora haziwezi kusaidia.”
Anaeleza kuwa wakulima wanaweza kuvuna kila tone la mvua kupitia mifumo ya kuvuna maji ya paa, mabwawa, na visima, mbinu ambazo tayari zimeonyesha mafanikio katika kaunti kama vile Kitui na Makueni.

Mtaalamu huyu wa masuala ya kilimo anashauri Wakenya kutumia vyema maji yaliyo majumbani mwao, akihoji hata yanayotumika kwa minajili ya usafi na shughuli zingine za nyumbani yanaweza kusafishwa kiteknolojia kuondoa viini na yakatumika kuzalisha chakula.
“Hata maji ya nyumbani yaliyotumika, kama ya kufulia, yanaweza kusaidia kuboresha mabustani madogo ya kilimo,” anaongeza.

Omondi anasisitiza pia umuhimu wa kukumbatia mazao, yaliboreshwa kijeni (genetics).
“Mazao yanayostahimili ukame kama vile mtama, mawele (ndio wimbi), ndengu, kunde, mihogo, viazi vitamu na mboga asilia ni muhimu sana. Yanahitaji maji kidogo, hukomaa haraka na yanazalisha chakula kwa wingi na vilevile yana mapato,” anasema.
Mbinu za kilimo hifadhi, kwa Kiingereza ndio conservation agriculture kama kulima kidogo bila kusumbua udongo, kufunika udongo kwa mabaki ya mazao na kupanda kwa kuchanganya mimea wakati wa upanzi, husaidia udongo kuhifadhi unyevuunyevu kwa muda mrefu.

Aidha, kuunganisha kilimo cha mimea na ufugaji – kwa kufuga mifugo kama mbuzi aina ya Galla na kondoo wa Red Maasai hupunguza athari za ukame kwani mkulima atapata mbolea kuboresha mazao.
Kwa wakulima wa mashamba madogo, mfano wenye kiwango cha shamba kama nusu ekari, Omondi anakadiria kuwa mfumo wa umwagiliaji maji kwenye mashamba na mimea kwa kutumia mifereji, ndio irrigation, unaweza kugharimu kuanzia Sh70,000. “Uvunaji wa maji ya mvua unaweza kugharimu kati ya Sh50,000 na Sh100,000, na ikumbukwe kuwa huu ni uwekezaji wa muda mrefu,” anasema.
Mtaalamu huyu anahimiza matumizi ya pampu za sola, akisema ni nafuu kwa muda mrefu na rafiki kwa mazingira.
Kuhusu pengo kufanikisha teknolojia kwenye zaraa, Omondi anaamini ushirikiano ni muhimu.

“Wakulima wakijiunga kwenye vikundi au vyama vya ushirika, watapata mikopo kwa urahisi, ikiwa ni pamoja na kupokezana maarifa na kupunguza gharama.”
Anaongeza kuwa sera thabiti, ruzuku kwa pembejeo za kilimo na mikopo ya bei nafuu ni muhimu ili kufanikisha ajenga ya kugeuza Kenya kuwa Israili ya kilimo.
Isitoshe, Omondi ataja vijana kama nguzo kuu kwenye sekta ya kilimo na ufugaji.
Vijana wanaweza kufanya kilimo kuwa cha kisasa, chenye faida na kinachovutia. Teknolojia ndiyo ufunguo wa mustakabali wa mifumo yetu ya chakula, anaelezea.
