Kimataifa

‘Makomandoo wanne’ wamuua Saif Al-Islam, mwanawe Gaddafi, Libya

Na MASHIRIKA February 4th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

TRIPOLI, LIBYA

SAIF al-Islam Gaddafi, mwana wa kiongozi wa zamani wa Libya, Kanali Muammar Gaddafi, ameripotiwa kupigwa risasi na kuuawa.

Kifo cha mwanasiasa huyo mwenye umri wa miaka 53, ambaye hapo awali alionekana kuwa mrithi wa baba yake, kilithibitishwa na mkuu wa timu yake ya kisiasa kulingana na Shirika la habari la Libya.

Wakili wake alisema kwamba mwanasiasa huyo aliuawa nyumbani kwake katika jiji la Zintan na kikosi cha “makomandoo wanne”.

Hata hivyo, haijabainika ni nani aliyehusika na shambulio hilo.

Kulikuwa na uvumi kwamba wanamgambo walio karibu na serikali yenye makao yake mjini Tripoli inayoongozwa na Waziri Mkuu Abdul Hamid Dbeibeh wamehusika na mauaji hayo, ingawa wenyewe wamekanusha.

Hata hivyo, dadake alitoa taarifa kinzani akiambia televisheni ya Libya kwamba alifariki karibu na mpaka wa nchi hiyo na Algeria.

Saif al-Islam Gaddafi kwa muda mrefu alionekana kuwa na ushawishi mkubwa na aliyeheshimiwa zaidi nchini baada ya baba yake, ambaye alitawala Libya kuanzia 1969 hadi alipoondolewa madarakani na kuuawa wakati wa uasi mwaka 2011.

Alizaliwa mwaka wa 1972 na kuchukua jukumu muhimu katika uhusiano wa Libya na nchi za Magharibi kuanzia mwaka wa 2000 hadi Gaddafi alipoondolewa madarakani.

Baada ya kuondolewa kwa babake, Saif al-Islam Gaddafi – ambaye alishutumiwa kwa kuwakandamiza waandamanaji waliokuwa wakiipinga serikali yake alifungwa jela na wanamgambo wapinzani katika jiji la Zintan karibu miaka sita.

Mahakama ya Kimataifa ya Jinai ilitaka kumshtaki kwa uhalifu dhidi ya ubinadamu kwa madai ya kuwakandamiza waliokuwa wakiandamana kuipinga serikali mwaka wa 2011.

Saif al-Islam Gaddafi, amekuwa na mvutano wa kisiasa na kisheria kwa zaidi ya muongo mmoja tangu mapinduzi ya 2011.

Wakati huo, mawakili wake walieleza hofu kuwa kesi dhidi yake nchini Libya haikuwa ya kusaka haki bali kisasi.

Kwa mujibu wa Umoja wa Mataifa, watu 15,000 waliuawa wakati wa mapigano ya kumng’oa Gaddafi, huku Baraza la Kitaifa la Mpito (NTC) likikadiria idadi hiyo kufikia 30,000.

Mwaka 2014, Saif al-Islam alifika mahakamani Tripoli kwa njia ya video akiwa kizuizini mjini Zintan.

Mwaka mmoja baadaye, Julai 2015, alihukumiwa kifo bila yeye kuwepo mahakamani.

Hata hivyo, mwaka 2017 aliachiliwa huru na kundi la wanamgambo la Abu Bakr as-Siddiq Battalion lililokuwa likidhibiti Zintan.

Licha ya kuachiliwa kwake, Saif al-Islam aliendelea kutafutwa na Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu (ICC) na hakujitokeza hadharani kwa miaka kadhaa.

Mnamo Julai 2021, alihojiwa na The New York Times, akizishutumu mamlaka za Libya kwa “kuogopa uchaguzi.”

Alisema amekuwa “mbali na watu wa Libya kwa miaka 10,” akieleza kurejea kwake.

Novemba 2021, alijitokeza hadharani kwa mara ya kwanza baada ya miaka kadhaa, mjini Sebha, alipowasilisha ombi la kugombea urais Libya, jaribio la kufufua uungwaji mkono wa wafuasi wa zamani wa baba yake.

Ingawa awali alizuiwa kushiriki, baadaye alirejeshwa kwenye kinyang’anyiro.

Hata hivyo, uchaguzi huo haukufanyika kutokana na misukosuko ya kisiasa, huku serikali mbili pinzani zikiwania madaraka nchini humo.

Saif al-Islam alikuwa mstari wa mbele katika kutoa wito wa mageuzi ya kisiasa, na alionekana kuwa mojawapo wa watu ambao walisukuma juhudi za kurekebisha uhusiano kati ya Libya na mataifa ya Magharibi kuanzia mwaka 2000 hadi mwanzo wa uasi wa mwaka 2011.