Tiketi ya dhahabu? Katibu Mkuu wa UDA kumenyana kwenye mchujo na mbunge wa zamani Ali Mbogo
ALIYEKUWA Mbunge wa Kisauni, Bw Ali Mbogo, atashindania tikiti ya chama cha UDA dhidi ya aliyekuwa seneta, Bw Hassan Omar, kuwania ugavana Mombasa mwaka wa 2027.
Wawili hao ni miongoni mwa wanasiasa zaidi ya 12,000 wanaopanga kushindania tikiti ya UDA kuwania nyadhifa mbalimbali katika uchaguzi mkuu ujao.
Hii itakuwa mara ya tatu kwa Bw Omar, ambaye ndiye Katibu Mkuu wa UDA, kuwania ugavana Mombasa. Aliwania kwa mara ya kwanza mwaka wa 2017 kwa chama cha Wiper, kisha baadaye 2022 kupitia UDA bila kufaulu.
Kwa upande mwingine, Bw Mbogo alipewa tikiti ya kuwania ugavana na chama cha Wiper mwaka wa 2022, lakini uamuzi huo ukabadilika baadaye ilipoamuliwa awe mgombea mwenza wa aliyekuwa gavana wa Nairobi, Bw Mike Sonko.
Hata hivyo, hatua hiyo ilipata pigo wakati Tume ya Uchaguzi (IEBC) ilipoamua Bw Sonko hakuhitimu kuwania kiti chochote cha kisiasa kwa sababu aling’olewa mamlakani kwa kukosa uadilifu.
Katika Kaunti ya Kilifi, aliyekuwa Spika wa Bunge la Kaunti, Bw Jimmy Kahindi, ameomba kuwania kiti cha ugavana kupitia UDA.
Awali, aliyekuwa Mbunge wa Malindi, Bi Aisha Jumwa, alitarajiwa kuwania tikiti hiyo lakini akahamia Chama cha Pamoja African Alliance (PAA).
Uamuzi wa Bi Jumwa unaaminika kusababishwa na jinsi baadhi ya viongozi wa UDA katika kaunti hiyo wameamua kumpigia debe Gavana Gideon Mung’aro wa ODM kwa awamu ya pili.
Msimamo wa wanasiasa hao, wakiongozwa na Mbunge wa Kilifi Kaskazini, Bw Owen Baya, unaashiria uwezekano wa UDA kutokuwa na mgombea ugavana Kilifi.
Lamu, aliyekuwa Mwenyekiti wa Tume ya Kitaifa ya Huduma za Polisi (NPSC), Bw Eliud Kinuthia Ndungu, na aliyekuwa seneta, Bw Anuar Loitiptip wamewasilisha maombi ya kuwania ugavana kupitia UDA.
Bw Ndungu aliwahi kuwania ugavana 2017 kupitia PNU lakini akajiondoa kwenye kinyang’anyiro baadaye.
Gavana wa Lamu, Bw Issa Timamy, anayehudumu awamu yake ya pili, amekuwa akimpigia debe naibu wake, Dkt Mbarak Mohamed Salim almaarufu Bahjaj, kurithi wadhifa huo.
Katika Kaunti ya Taita Taveta, aliyekuwa gavana Granton Samboja na Katibu wa Wizara ya Leba Shadrack Mwadime wameomba kuwania tikiti ya UDA ya ugavana.
Bw Samboja alishinda ugavana 2017 kupitia Wiper ila akahamia chama cha Jubilee kuwania kiti hicho 2022 bila mafanikio.
Gavana wa Kwale, Bi Fatuma Achani, anatarajiwa kushindania tikiti hiyo dhidi ya naibu wake, Bw Chirema Kombo.