Maoni

MAONI: Mafanikio ya ajenda za serikali yagubikwa na kampeni za 2027

Na PAUL NABISWA February 5th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

TUMESALIA na mwaka mmoja kabla ya uchaguzi mkuu wa 2027 ila mikimbio ya wanasiasa imekuwa mingi kuliko uhalisia wa hali.

Rais William Ruto anaongoza upande wa serikali kupata muhula wake wa pili.

Muungano wa upinzani nao umo mbioni kuhakikisha kuwa Ruto anaiona ikulu kwa paa kipenga cha uchaguzi wa 2027 kitakapopulizwa. Wananchi wamesalia katikati.

Kenya ina mfumo wa kuwa na uchaguzi kila baada ya miaka mitano lakini katika mazingira ya sasa, anayelala pia hataingia anapotaka parapanda ya uchaguzi itakapolia.

Athari ya hali kama hii ni kuwa pande zote zinaibuka na chuku ili kuboresha tamthilia yao ya uchaguzi wa 2027.

Kwa mfano, mradi wa nyota ambao unawafaa vijana kwa mikopo ni mzuri tu ila haujaeleweka na wengi kikamilifu kwa sababu ajenda kubwa imekuwa kuuza jina la Rais na kusahau mafanikio ya moja kwa moja kwa wafaidi.

Inapotukia hivi, wakati mwingine walengwa hukosa kutathmini masuala ya sera na kujipata katika ushabiki.

Mawaziri katika serikali ya Rais Ruto na wafanyikazi wa serikali wameamua ni siasa “bila break” jinsi wanavyonadi matamanio ya Rais kupewa muhula mwingine.

Hapa swali kuu ni je, hawa mawaziri na wakuu serikalini wanafanya kazi afisini saa ngapi na kila wakati wamo katika miradi ya serikali hata ile isiyowahusu moja kwa moja?

Si hayo tu, serikali imejipata katika mkanganyiko mkubwa, hata kata hiyo mikutano siasa za serikali jumuishi zimeshika kazi.

Kwa mfano, mwenyekiti wa chama cha ODM Gladys Wanga amesema tayari kuwa muungano wao unataka mgao wa nusu bin nusu na UDA.

Hili linaweza kuleta mtafaruku na watu wengine ambao pengine walikuwa na madhumuni ya kufanya kazi na Rais Ruto kwa sababu wataonekana kuwa tayari wamefungiwa nje.

Kazi kubwa ingekuwa kwa wanasiasa kuwashauri watu kujisajili kuwa wapiga kura, wajibu ambao wameshindwa.

Tume ya Uchaguzi na Mipaka imekuwa ikiwapokea Wakenya wachache mno vituoni katika shughuli ya kuwasajili wapiga kura.

Upinzani pia umekuwa na mambo mengi tu, mikutano ya hadhara kwa dharura na kuilamu serikali.

Baadhi ya washirika hawajakuwa wakitoa suluhisho kwa masuala tata yanayoikumba nchi badala yake kulazimisha mijadala ya kitaifa kwa mambo ya kibinafsi.

Sababu kuu ya kuwa na vituko hivi vya siasa ni kuwa, vyama vya siasa havina itikadi maalumu.

Serikali inakosoa upinzani bila hoja bali inazingatia mabavu yake ya kukalia kiti. Upinzani nao wanachukulia tu kuwa unachukiwa na serikali katika harakati zao.

Hii ngoma ni nzito na itawabidi wadau wajitambue.

Paul Nabiswa ni mhariri, NTV