Kimataifa

Trump akataa kuomba radhi kuhusu video ya kubagua familia ya Obama

Na REUTERS February 8th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

RAIS Donald Trump alilaani bila kuomba radhi kufuatia video iliyochapishwa kwenye akaunti yake ya iliyoonyesha aliyekuwa Rais wa Amerika Barack Obama na mkewe Michelle Obama kama nyani, chapisho lililokosolewa vikali na pande zote za kisiasa kwa kudhalilisha watu wenye asili ya Kiafrika.
Ikulu ya White House Ijumaa ilitetea chapisho hilo la kibaguzi kabla ya kulifuta saa 12 baadaye.
Video hiyo ya takriban dakika moja, iliyochapishwa katika mtandao wa Truth Social unaomilikiwa na Trump Alhamisi usiku, ilisambaza madai ya uongo kwamba kushindwa kwake katika uchaguzi wa 2020 kulitokana na udanganyifu.
Mwishoni mwa video hiyo kulikuwa na kipande kifupi kinachodaiwa kuundwa na teknolojia ya Akili Unde (AI), kikionyesha nyani wakicheza huku nyuso za familia ya Obama zikiwa zimebandikwa.
Akizungumza na wanahabari Ijumaa usiku, Trump alisema hakutazama video nzima kabla ya msaidizi wa Ikulu kuichapisha.
“Sikuiona yote. Niliona sehemu ya mwanzo tu, iliyohusu madai ya udanganyifu wa kura,” alisema.
Alipoulizwa kama analaani kipande hicho, Trump alisema: “Bila shaka nakilaani,” lakini alikataa kuomba radhi akisema hakufanya kosa.
Kauli za Trump zilijiri huku kukiwa na mkanganyiko ndani ya Ikulu.
Msemaji mmoja wa utawala awali alitetea video hiyo akisema ni “kejeli ya mtandaoni isiyo na madhara,” kabla ya afisa mwingine kusema ilichapishwa kimakosa na kuondolewa.
Trump, ambaye yuko katika muhula wake wa pili, ana historia ya kutoa kauli na machapisho yanayochukuliwa kuwa ya kibaguzi.
Kwa muda mrefu alieneza nadharia ya uongo kwamba Obama, aliyekuwa rais kati ya 2009 na 2017, hakuzaliwa Amerika.
Chapisho hilo lilikosolewa vikali na chama cha Democratic na baadhi ya wanachama wa chama chake cha Republican, akiwemo Seneta Tim Scott wa South Carolina, mshirika wa karibu wa Trump.
“Naomba iwe ni bandia tu kwa sababu ni kitu cha kibaguzi zaidi ambacho nimeona kutoka Ikulu hii,” Scott aliandika katika mtandao wa X.
Kwa karne nyingi, watu wenye itikadi za ubaguzi wa rangi wamekuwa wakiwafananisha Waafrika na nyani kama njia ya kuwadhalilisha.
“Historia itamkumbuka Obama kama kiongozi mpendwa, huku Trump akichukuliwa kama doa katika historia,” alisema Ben Rhodes, aliyekuwa msaidizi wa Obama.
Msemaji wa familia ya Obama alikataa kutoa maoni.
Wachambuzi na wanaharakati wa haki za binadamu wanasema lugha na matamshi ya Trump yamekuwa yakizidi kuwa makali.
“Video ya Donald Trump ni ya kibaguzi waziwazi, ya kuchukiza na isiyokubalika,” alisema Derrick Johnson, rais wa NAACP.
“Wapiga kura wanaangalia na watakumbuka haya siku ya kupiga kura.”