Shabiki sugu wa United aliyeapa kutonyoa nywele sasa atafuta kinyozi
MANCHESTER United walishinda Tottenham Hotspur ugani Old Trafford Jumamosi na kuweka hai matumaini ya shabiki wao sugu kunyoa nywele, hatimaye.
Frank Ilett, 29, amekaa kwa takriban siku 500 bila kunyoa nywele baada ya kuapa kutofanya hivyo mnamo Oktoba 5, 2024 hadi wakati United watashinda mechi tano mfululizo.
Lakini kusuasua kwa miamba hao wa zamani wa Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) mwanzo wa msimu huu kumeacha shabiki huyo na shungi la nywele anazozifuga kwa mtindo wa ‘afro’.
Sasa wachezaji wa Man United wanatarajiwa kuendeleza ubabe wao baada ya kukomoa Manchester City (2-0), Arsenal (3-2), Fulham (3-2) na Spurs 2-0 wakiwa chini ya kocha mshikilizi Michael Carrick.
Umebaki ushindi mmoja pekee kwa Ilett kufaulu kukata shungi la nywele lililojaa kichwani.
Ushindi dhidi ya Spurs na West Ham United mnamo Jumanne utafanya Man-United kumpa Ilett nafuu ya kunyoa nywele zake mwishowe.