Kinaya msemaji wa Museveni kudai wanachunguza uvamizi katika makazi ya Bobi Wine
KAMPALA, UGANDA
WAZIRI wa Habari nchini Uganda, Chris Baryomunsi, ameshutumu hatua ya jeshi ya kuvamia nyumbani ya Kiongozi wa Upinzani Robert Kyangulanyi maarufu kama Bobi Wine.
Baryomunsi alisema kuwa mwanasiasa huyo hajatekeleza uhalifu wowote na yupo huru kurejea katika makazi yake.
Wine amekuwa mafichoni kwa wiki kadhaa baada ya kutoroka nyumbani kwake jijini Kampala, saa chache baada ya Yoweri Museveni kutangazwa mshindi wa uchaguzi mkuu wa Januari 15.
Museveni, 81 alitangazwa mshindi wa uchaguzi huo kwa asilimia 71.6 za kura huku Kyangulanyi akipata kura milioni 2.7.
Mnamo Januari 31, 2026, Museveni alidai kuwa mpinzani wake Bobi Wine alichapisha kura milioni moja feki na nyingine milioni 1.7 kutoka Dubai ili kupata ushindi kwenye uchaguzi mkuu wa Januari 17.
Kwa upande mwingine, alisema kuwa kutumika kwa mfumo wa kielektroniki kwenye uchaguzi huo ndiko kulizuia njama ya upinzani kutumia njia ya udanganyifu katika kura hiyo.
Alidai kuwa kwa sasa hakuna upinzani Uganda kwa sababu wapigakura wameonyesha imani yao kwa kumpa kura kupitia NRM.
“Fahamu hakuna upinzani Uganda, hao wanaosema kunao wanajidanganya tu. Baada ya uchaguzi tuligundua walichapisha karatasi milioni moja za kupiga kura hapa barabara ya Nkuruma na milioni nyingine milioni 1.7 kutoka Dubai,” Museveni alisma.
Kiongozi alisifu matumizi ya mitambo ya kielektroniki ya kupiga kura akisema ilimwokoa kushindwa kwa njia ya udanganyifu na Kyangulanyi.
Kando na hayo, aliwakashifu viongozi hao wa upinzani kwa kulenga familia yake.
Mnamo Januari 24, Wine alisema mkewe alikuwa amepelekwa hospitalini baada ya wanajeshi kuvamia makazi yao akidai walimvua nguo na kumnyonga.
Mkuu wa jeshi la Uganda Muhoozi Kainerugaba ambaye ni mwanawe Museveni alikanusha kuwa wanajeshi walimdhulumu mkewe Wine akisema alinyakwa kisha akaachiliwa huru.
Baryomunsi ambaye pia ni msemaji wa serikali alisema wanachunguza tukio hilo.
“Hatuvumilii tukio lolote la ukosefu wa nidhamu upande wa jeshi na maafisa wa usalama. Kwa hivyo, kuvamia boma la Wine kumesababisha uharibifu na pia kumdhulu mkewe au mtu yoyote ni makosa,” akaongeza.
Hata hivyo, alikataa kusema iwapo maafisa wa usalama watakabiliwa na adhabu yoyote iwapo watapatikana wamevunja sheria.
Kainerugaba ametangaza mitandaoni kuwa wanajeshi wanamsaka Wine ambaye anapinga matokeo ya uchaguzi wa urais akidai kuwa kulikuwa na udanganyifu.
Mkuu huyo wa jeshi hata hivyo hajasema kwa nini wanamsaka Wine au kitendo chochote cha uhalifu ambacho ameshiriki.
Makundi mbalimbali yameshutumu Museveni ambaye amekuwa mamlakani kwa kipindi kirefu kwa kutumia jeshi kuwaandama wakosoaji wa serikali.
Hata hivyo, serikali imeyakanusha madai hayo.
Baryomunsi pia alisema Uganda haina mpango wa kuwaondoa wanajeshi wake kutoka Muungano wa Umoja wa Afrika ili wapambane na magaidi Somalia.
Wiki jana Kainerugaba kupitia mtandao wa X alichapisha kwamba Uganda itawaondoa wanajeshi wake Somalia kutokana na masuala ya kifedha.
Kainerugaba ana mazoea ya kuchapisha jumbe tata mitandaoni kisha huwa kuzifuta baadaye.
Aliwahi kutishia kuwa atamkata Wine kichwa na akajigamba kuwa jeshi lilikuwa limewaua wafuasi 30 wa upinzani.
Baryomunsi alisema kuwa jumbe za Kainerugaba zinastahili kuchukuliwa kama yake binafsi wala si kama yaliyotolewa na serikali ya Uganda.